BALOZI wa Norway nchini, Ingunn Klepsvik ameonya kuhusu hatari za kugeuza suala la gesi ya Mtwara kuwa mtaji wa kisiasa.
Wakati Norway ikisema hayo, Mkurugenzi wa Uchumi katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Dk Nyamajeje Weggoro amesema mgogoro huo utamalizika kwa njia ya mazungumzo na majadiliano yaliyojaa lugha na kauli laini isiyo na vitisho wala kuwabeza wananchi.
Katika siku za karibuni, kumekuwa na mijadala, mizozo na maoni kutoka kwa kada mbalimbali kuhusiana na suala la gesi hiyo inayopatikana katika eneo la Msimbati, Mtwara.
Akitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Sebastian Kolowa, Lushoto mkoani Tanga, Balozi Klepsvik alisisitiza kuhusu haja ya Watanzania kuweka mbele masilahi ya taifa badala ya kuangalia masilahi ya watu binafsi au taasisi.
“Norway ilipogundua nishati ya petroli tulikubaliana kitu kimoja kwamba suala hili lisihusishwe na kampeni za kisiasa. Hii itasaidia kuweka mbali masuala ya rasilimali na siasa,” alisema.
Balozi huyo alisema gesi ya Mtwara inapaswa kuwanufaisha wananchi wa Mtwara kwanza kabla ya watu wengine, lakini masilahi ya taifa lazima yawekwe mbele katika mjadala wa suala hilo.
Klepsvik alisisitiza kuhusu umuhimu wa kuwashirikisha wananchi katika masuala muhimu ya maendeleo na kueleza kuwa maendeleo endelevu yanapatikana kwa kuwahusisha watu wa kada zote hasa wanawake.
Hata hivyo, alisema endapo mambo yatafanyika kwa utaratibu wake, gesi iliyovumbuliwa inaweza kuwasaidia Watanzania kwa kiasi kikubwa katika maendeleo yao.
“Tulipogundua gesi na petroli, hatukuwa tunafahamu lolote, tuliita wageni wakatufanyia kazi ya kuchimba, wakati huo tulipeleka watu wetu vyuo vya nje kusoma na baada ya miaka 10 sasa tunashughulika wenyewe na kila kitu kwa manufaa ya taifa zima,” alisema Klepsvik.
EAC yashauri mazungumzo
Akizungumzia mgogoro huo, Dk Weggoro alisema umetokana na wananchi kutopata elimu ya kutosha kuhusu namna watakavyofaidika na rasilimali hiyo inayopatikana katika eneo lao.
EAC yashauri mazungumzo
Akizungumzia mgogoro huo, Dk Weggoro alisema umetokana na wananchi kutopata elimu ya kutosha kuhusu namna watakavyofaidika na rasilimali hiyo inayopatikana katika eneo lao.
“Mgogoro wa gesi Mtwara utamalizika kwa njia ya mazungumzo na majadiliano lakini siyo vitisho,” alisema alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya EAC jana.
Alisema haamini kama ni kweli wananchi wa Mtwara hawataki Watanzania wenzao wafaidike na gesi inayopatikana mkoani humo, bali wanahofia hatima ya maisha, faida na masilahi yao kutokana na rasilimali hiyo.
“Viongozi lazima wazungumze, wajadiliane na kufikia mwafaka na wananchi (wanaMtwara), kuhusu mambo yanayogusa maisha na masilahi yao. Ni vyema watu ambao maliasili na rasilimali zinapatikana katika maeneo yao wanufaike kwanza kabla ya wengine.”
Soma zaidi.....Mwananchi
No comments:
Post a Comment