Pages

Wednesday, July 31, 2013

Mambo ya kuangalia katika kuanzisha Mradi


Habari wanablog:

Hakika kwa yeyote anayetaka kuanzisha biashara yampasa kuwa makini na aina ya biashara anayotaka kuanzisha. Kumbuka lengo la kuanzisha biashara (mradi) ni kujipatia faida ama kuhakikisha mteja anaridhika na kile anachokipata. Kuna mambo ya msingi kadhaa ambayo mjasiriamali anaweza kutumia kama muongozo katika kuanzisha mradi mpya.

Uainishaji wa Fursa (opportunity identification)

Kabla hujaanzisha mradi jambo la muhimu na la msingi ni kuainisha fursa zilizopo katika eneo linalokuzunguka. Fursa ni mazingira chanya na saidizi ambayo mjasiriamali anatumia kuanzisha mradi na kujipatia faida nyingi kwa muda mfupi ama mrefu. Mara tu mjasiriamali anapotambua fursa zilizopo na kuamua kuanzisha mradi, akijua kuwa matarajio ya mradi huo ni chanya basi mjasiriamali huyo uwekezaji wake una matarajio yafuatayo.
  • Mradi kuwa na mapato mazuri na endelevu
  • Mradi kuwa na soko la uhakika
  • Gharama za uendeshaji wa mradi kuwa nafuu
  • Mradi kuwa na uwezekano wa kukua.
Utakapojiridhisha kuwa hayo ya juu yanaweza kudhihiri, basi unaweza kuwekeza na kuanzisha mradi wa bidhaa ama utoaji huduma, kwa sababu kuna uwezekano mkubwa wa upatikanaji wa faida.
 
Vyanzo vya utambuzi wa fursa
 
  • Mabadiliko ya teknolojia- hapa tumeona jinsi makundi mbalimbali yalivyofaidika na mabadilikoya teknolojia..Mfano watu wamejiajiri kupitia huduma za simu na kujipatia faida kupitia M-pesa, Tigo-pesa, Airtel money.....zamani fursa hizi hazikuepo. Pia kuna blogs za kibiashara mbali mbali zimeanzishwa nia na lengo ni kujipatia kipato kupitia kwa wadhamini: Mfano Mjengwa blog, Michuzi blog na jamii forum. Bado hujachelewa fursa zinazopatikana juu ya mabadiliko ya teknolojia zipo nyingi na kwenye sekta tofauti tofauti.
 
  • Uelewa- Kwenye jamii yoyote uelewa wa mambo unapoongezeka huambatana na fursa mbali mbali za kiuchumi zinazoendana na kuongezeka kwa uelewa. Mathani mahitaji ya vyakula vilivyo salama na kemikali umekuwa mkubwa, kulinganisha na vyakula vinavyotokana na kemikali, hii ina sababishwa na watu kuwa na elimu juu ya madhara ya kemikali mwilini.
 
  • Mabadiliko ya sera-
Itaendelea: Niandikie mmlanzi@yahoo.com
 

Monday, July 29, 2013

Mradi ama biashara (Enterprise)


Habari wana blog:

Leo tunaendelea na mada yetu ya ujasiriamali baada ya kuwa katika mapumziko ya mwisho wa wiki, kwa kujifunza nadharia ya mambo mbalimbali yanayopatikana kwenye ujasiriamali. Chapisho la mwisho tuliona sifa mbali mbali za mjasiriamali kinadharia. Leo hii tunaenda kuangalia biashara ama miradi ambayo mjasiriamali anaweza kijishughulisha nayo ili aweze kutimiza lengo lake lake la kujipatia faida na kumridhisha mteja. Kumbuka huwezi fanya jambo lolote kwa ufasaha zaidi kama hujui nadharia ya jambo hilo kwa ufasaha zaidi.
 
Mradi/Miradi ni nini?
Kwa lugha ya kijasiriamali Mradi ni biashara unayoitekeleza (commercial untertaking) ima kuzalisha bidhaa ama kutoa huduma kwa lengo la la kujipatia faida na kuridhisha wateja. Takwimu zinaonesha kuwa asilimia kubwa ya watanzania wanajishughulisha na kilimo. Kilimo hapa ni neno pana kwa maana ya uzalishaji wa mazao mfano: Mahindi, Mpunga (Mchele), viazi na mazao mengine mbali mbali unayoyafahamu, matunda, mbogamboga na maua.
 
Pia kilimo kinahusu ufugaji wa wanyama mbali mbali mfano: Ng'ombe, Mbuzi, Nguruwe na Kondoo:Ufugaji wa ndege Mfano: Kuku, bata, njiwa na kanga. Ufugaji huwa na lengo la uzalishaji wa bidhaa kama nyama, ngozi, maziwa, mayai na bidhaa nyingine zitokanazo na wanyama ama ndege.
 
Kwa hiyo mradi unaweza kuwa ni uzalishaji wa bidhaa kama tulivyoona hapo juu, pia mradi unaweza kujikita kwenye utoaji huduma. Mathalani afisa ugani ambaye ana taaluma ya utabibu wa mifugo anaweza kutibu mifugo kumi mpaka ishirini kwa siku na kulipwa ujira kwa kutoa huduma hiyo. Kuna huduma nyingi hutolewa na kisha ujira hutolewa baada ya huduma hiyo kupatikana. Mfano wa huduma hizo ni Ufundishaji (elimu), mawasiliano, ushauri, matengenezo, ufundi, usafirishaji , udalali n.k.
 
Somo tunaloweza kujifunza hapa ni kwamba mjasiriamali ana wigo mpana wa kuchagua aina ya mradi anaotaka kuutekeleza, aidha azlishe bidhaa ama atoe huduma. Miradi hii hutofautiana kulingana na mtaji uliowekezwa kwenye mradi husika na kufanya miradi hyo iwe ya aina mbili aidha midogo (micro enterprise) ama mikubwa (Macro enterprise).
 
 
Itaendelea: niandikie mmlanzi@yahoo.com
 
 

Friday, July 26, 2013

Mjasiriamali na Mfanyabiashara


Habari wana blog:

Chapisho la mwisho tuliona kwa ufupi na maana nyepesi ya neno ujasiriamali na kuangalia jinsi mjasiriamali anavyowezesha kutumia rasilimali ardhi, watu, maji na mtaji kuweza kufanya uzalishaji aidha wa mazao (bidhaa) ama kutoa huduma kwa lengo la kujipatia faida.
 
Ubunifu
Bado neno Mjasiriamali linaweza kuwa na maana nyingi ikiwemo ya uwezo wa mtu (mfanyabiashara) kubuni (innovations) kitu (vitu) vipya na kuvitambulisha katika jamii inayomzunguka katika jitihada ya kufanya vitu hivyo viwe na uwezo wa kujikwamua kiuchumi.
 
Kumbuka sio wafanyabiashara wote ni wajasiriamali, ila wajasiriamali wote ni wafanyabishara. Sifa mojawapo ya mjasiriamali ni kuwa mbunifu wa vitu vipya (bidhaa ama huduma). Huduma kama njia mojawapo ya kupata faida ni kama vile haifahamiki miongoni mwa watanzania wengi. Wengi wetu hufikiri ili uweze kupata kipato ni vyema ukauza bidhaa, huku utoaji wa huduma ukiachwa kwa watu wachache ambao hutumia fursa hiyo kupata faida kubwa.
 
Hivyo ubunifu huweza kusababisha biashara mpya kujitokeza na kuajiri ama kutumika kama ajira binafsi kwa msururu wa wafanyabishara wengine (duplication). Hapo juu tumeona kuwa si wafanyabiashara wote ni wajasiriamali, ila wajasirimali wote ni wafanyabiashara. Hii ni kwa sababu mjasiriamali ana sifa za ziada na za kipekee kumshinda mfanyabiashara.

Sifa hizi za ziada za mjasiriamali ni Mbunifu (innovator), kujitegemea (independent), kujiamini (self-confidence), mpangiliaji (organized), muono (vision), sugu (persistent), Tumaini (optimism), commited, mtendaji (action-oriented), mtatuzi wa matatizo (problem solver), kujihusisha na hatari: kutoogopa kupata hasara (risk taker) na anayenyumbulika (flexiblity).

Sifa hizi ni za mjasiriamali aliyekamilika na aghalabu kukuta mfanyabiashara kuwa nazo. Usihofu kama hauna kipaji cha ubunifu, unaweza kuiga mambo mazuri kutoka kwa wabunifu na ukayatumia ili uweze kujikwamua kuchumi.
 
Itaendelea
 
 Unaweza kukomenti kwenye hii blog :

 Ama niandikie maboresho kwenye mmlanzi@yahoo.com
 

Thursday, July 25, 2013

Ujasiriamali ni nini?

Wapenzi wa blog hii nimeamua kubadili mfumo wa blog hii kutoka katika kuleta taarifa mbali mbali za kijamii na kujikita zaidi na dhana nzima ya ujasirimali. Blog hii itakuwa inakuletea tips mbalimbali za ujasiriamali kwa kadiri ya uwezo utakavyokuwa unapatikana. Hivyo nategemea mafunzo mengi pia kutoka kwa wasomaji wa blog hii ili tuweze kuondoka katika mzunguko huu wa umasikini.
 
 Lengo kuu ni kusaidia watanzania wenzangu kujua mbinu mbalimbali zinazotumiwa na wafanyabiashara mbali mbali kupata mafanikio ya kibiashara, kutumia mbinu hizo kwa kuiga ama kuibua mbinu mbadala ili tuweze kuondokana na umaskini.
 
Huku idadi ya watu ikizidi kuongezeka duniani na Nchini kwetu kwa ujumla, changamoto kuu imekua suala la ajira. Kila mmoja wetu anataka kuajiriwa aidha serikalini ama kwenye sekta binafsi huku suala la kujiajiri likiwa la mwisho katika vipaumbele.
 
Ujasiriamali ni nini?
 
Kwa sasa ni jina maarufu sana hapa Tanzania, mtu yeyote aliyefanikiwa katika biashara hupewa jina hili. Maana ya ujasirimali inabaki katika uwezo wa kufanya maamuzi sahihi wa kutumia rasilimali chache zinazokuzunguka vizuri ili uweze kupata faida.
 
Mathalani rasilimali zinazokuzunguka ni ardhi, watu na maji, ni vipi mchanganyiko huu utautumia vizuri ili uweze kupata zao (output) ambayo itakusaidia kujikwamua katika hali uliyonayo. Ama ni vipi utatumia mtaji mdogo ulionao kufanya biashara itakayokuletea faida ambayo utaitumia kuongeza mtaji na kuikuza biashara yako.
 
Fahamu kwamba lengo lolote la mjasiriamali ni kupata faida na kumridhisha mteja ambaye anatumia bidhaa ama huduma inayotolewa na mjasiriamali. Bidhaa ama huduma ndio msingi wa mjasirimali yeyote ambaye anataka kupata faida. Mathalani mkulima wa mahindi bidhaa yake ni mahindi hivyo atauza mahindi kujipatia faida, na mtabibu wa mifugo anatoa huduma ya matibabu kwa mifugo na kulipwa ujira kwa kutoa huduma hiyo.
 
Itaendelea....
 
Niandikie: mmlanzi@yahoo.com
 
 

Tuesday, June 4, 2013

Full: Hotuba ya Mh Jaji Sinde Warioba: Uzinduzi wa Rasimu ya Katiba Mpya!

 
HOTUBA YA MWENYEKITI WA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA, JAJI JOSEPH S. WARIOBA, KATIKA MKUTANO WA WAANDISHI WA HABARI KUHUSU UZINDUZI WA RASIMU YA KATIBA TAREHE 03 JUNI, 2013 KWENYE VIWANJA VYA UKUMBI WA KARIMJEE,
DAR ES SALAAM
.
Mhe. Dkt Mohammed Gharib Bilali – Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano,
Mhe. Mizengo K. P. Pinda (Mb.) – Waziri Mkuu,
Mhe. Seif Sharif Hamad – Makamu wa Kwanza wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Mhe. Balozi Seif Ali Iddi (Mb.) – Makamo wa Pili wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Mhe. Mathias Chikawe – Waziri wa Katiba na Sheria,
Mhe. Abubakar Khamis Bakary – Waziri wa Katiba na Sheria wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Mhe. Jaji Frederick M Werema – Mwanasheria Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Othman Masoud Othuman – Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar,
Viongozi wa Vyama vya Siasa,
Waheshimiwa Wajumbe wa Tume na Wajumbe wa Sekretarieti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba,
Ndugu Wananchi,
Wageni Waalikwa
Waandishi wa Habari Mabibi na Mabwana.

UTANGULIZI

Ndugu Wananchi,
Awali ya yote namshukuru mwenyezi mungu kwa kutuwezesha kufikia hatua hii ya leo ya kuzindua Rasimu ya Katiba. pia, niwashukuru ninyi nyote mliohudhuria halfa hii ikiwa ni mwendelezo wa mchakato muhimu wa Mabadiliko ya Katiba ya nchi yetu.

Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilipitishwa Bungeni Novemba, 2011 na kufanyiwa mabadiliko Februari, 2012. Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliundwa kwa mujibu wa Kifungu 6(1) cha sheria hiyo (Cap.83). Wajumbe 34 wa Tume waliteuliwa na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, mwezi Aprili, 2012. Kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Tume imepewa miezi kumi na minane kukamilisha kazi yake kuanzia siku ilipoanza kazi rasmi ambayo ilikuwa Mei 2, 2012.

Tume iliandaa ratiba ya utekelezaji wa majukumu yake. Kufuatana na ratiba hiyo Tume ilijipanga kukusanya maoni ya wananchi katika kipindi cha miezi mitano kuanzia Mwezi Julai hadi Disemba, 2012. Kazi hiyo ilifanywa kama tulivyopanga. Tume ilijigawa katika makundi na ilitembelea mkoa yote thelathini.

Tume ilifanya mikutano 1,942 ambayo ilihudhuriwa na wananchi wapatao 1,365,337 ambao kati ya hao wananchi 333,537 walitoa maoni ama kwa mazungumzo ya ana kwa ana au kwa maandishi. Tume pia ilipata maoni ya wananchi wengi, wa ndani na nje ya nchi kwa njia mbali mbali kama vile; Mikutano ya hadhara, Fomu maalum za Tume, barua kupitia Masanduku ya Barua ya Tume, Mitandao ya Kijamii ya barua pepe; facebook ya Tume, Tovuti ya Tume; Makala mbalimbali kutoka kwenye magazeti na ujumbe mfupi wa simu.

Tume ilitumia mwezi Januari, 2013 kukusanya maoni ya makundi mbali mbali katika jamii, ikiwa ni pamoja na vyama vya siasa, taasisi za Serikali, taasisi za dini, wakulima, wafugaji, wafanyakazi, asasi za kiraia na kadhalika. Makundi zaidi ya 160 yalikutana na Tume na kutoa maoni. Tume pia ilipata maoni ya viongozi wa juu wa Serikali walioko madarakani na waliostaafu. Kwa jumla viongozi 43walitoa maoni.

Tume ilipanga kutumia miezi mitatu ya Februari, Machi na Aprili kuchambua maoni ya wananchi na kuandaa Rasimu ya Katiba. Lakini tuligundua kwamba maoni tuliyopata yalikuwa mengi sana, na pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa, tulitambua umuhimu wa kuongeza muda hadi mwisho wa mwezi Mei, Maoni ya wananchi yaligusa mambo yote yanayohusu Katiba na mengi ya maoni hayo yalikinzana. Aidha, baadhi ya maoni yaligusia masuala ya Kisera, Kisheria na Kiutendaji. Tulifanya uchambuzi makini na wa ndani wa maoni hayo na kazi hiyo tumeikamilisha na rasimu imeandaliwa na Tume na leo tupo hapa kwa ajili ya kuizindua, ambapo Wananchi watapata nafasi ya kuisoma. Kwa leo, kwa niaba ya Tume, napenda kutaja maeneo machache tu ambayo tunayapendekeza.

IBARA ZINAZOPENDEKEZWA KWENYE RASIMU YA KATIBA

Ndugu Wananchi,
Katiba yetu ya sasa ina ibara 152. Tume ilifanya jitihada kubwa sana kuandaa rasimu ambayo siyo ndefu. Lakini katika hali halisi haikuwezekana. Rasimu ya Katiba tunayopendekeza ina ibara 240.

MISINGI MIKUU YA TAIFA

Utangulizi wa Katiba ya sasa ndio unaobeba misingi mikuu ya Taifa ambayo ni Uhuru, Haki, Udugu na Amani. Tume inaamini kwamba misingi hii ni mizito na inastahili kubaki kwenye Katiba mpya. Hata hivyo, Tume imeona ni busara kuongeza misingi mingine mitatu ya Usawa, Umoja na Mshikamano. Hivyo, Tume imependekeza Katiba iwe na Misingi Mikuu saba ya Taifa;yaani; Uhuru, Haki, Udugu, Usawa, Umoja, Amani na Mshikamano.

TUNU ZA TAIFA

Katiba yetu ya sasa haina sehemu inayoelezea tunu za Taifa (National Values). Wananchi wengi walitoa maoni kwamba Katiba itaje Tunu za Taifa. Tume imependekeza Tunu zifuatazo zitajwe ndani ya Katiba. Tunu hizo ni;- Utu, Uzalendo, Uadilifu, Umoja, Uwazi, Uwajibikaji na Lugha yetu ya taifa ya Kiswahili.

MALENGO YA TAIFA

Tume ilipozunguka nchi nzima wananchi walizungumzia sana kuhusu malengo ya taifa. Walitaka Katiba ionyeshe dira ya taifa. Wananchi wanayo ndoto yao ya Tanzania ya kesho na kesho kutwa. Kwa kuzingatia maoni ya wananchi, kuna sura nzima inayohusu Malengo mahsusi na ya msingi ya mwelekeo wa shughuli za Kiserikali na Sera za Kitaifa. Rasimu ya Katiba inaeleza kuwa Malengo ya Kitaifa yaliyoainishwa ndani ya Rasimu yatakuwa ni Mwongozo kwa Serikali, Bunge, Mahakama, Vyama vya Siasa, Taasisi na Mamlaka nyingine, na kwa kila mwananchi katika matumizi au kutafsiri Masharti ya Katiba au Sheria nyingine za Nchi.
Kwa msingi huo, Tume imependekeza malengo makuu ya taifa yapanuliwe kwa mpangilio wa kuonesha malengo ya kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutamaduni, kimazingira na sera ya mambo ya nje. Malengo hayo yameingizwa kwenye Rasimu ya Katiba.

VYOMBO VYA KIKATIBA

Wananchi walizungumzia suala la kubainishwa kwa vyombo vya Kikatiba na kuingizwa kwenye Katiba ili viwe na nguvu ya Kikatiba katika utekelezaji wa majukumu yao. Tume imependekeza baadhi ya vyombo vifuatavyo viwe vya Kikatiba; Tume ya Uhusiano na Uratibu wa Serikali, Baraza la Mawaziri, Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu na Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri; Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa, Tume Huru ya Uchaguzi, Tume ya Utumishi wa Mahakama, Tume ya Utumishi wa Umma, Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora

MAADILI YA VIONGOZI NA MIIKO YA UONGOZI

Wananchi wengi pia walizungumzia kwa upana sana kuhusu maadili na miiko ya Viongozi, kwa kuzingatia maoni ya wananchi Tume inapendekeza maadili ya viongozi wa umma, pamoja na miiko ya uongozi yawekwe kwenye Katiba. Tume pia imependekeza kuwa Sekretariati ya Maadili ibadilishwe kuwa Tume yenye mamlaka makubwa ya kusimamia maadili ya viongozi wanaovunja miiko ya uongozi.

HAKI ZA BINADAMU

Kuhusu haki za binadamu wananchi walitaka haki hizi ziimarishwe na kusiwe na vikwazo visivyo vya lazima. Tume imependekeza mabadiliko katika baadhi ya haki za binadamu kwa madhumuni ya kuziimarisha. Moja ya mabadiliko hayo ni kuhusu uhuru wa mwananchi kushiriki shughuli za umma. Tume inapendekeza kwamba vikwazo vilivyowekwa kuzuia mgombea huru viondolewe. Kwa maana nyingine Tume inapendekeza mgombea binafsi aruhusiwe.

Tume pia, inapendekeza haki mpya ziingizwe kwenye Katiba ikiwa ni pamoja na haki ya wafanyakazi, , haki ya mtoto, haki za Watu wenye Ulemavu, Haki za Wanawake, Haki za Wazee, Haki za Makundi Madogo katika Jamii, Haki ya Elimu na Kujifunza, Haki ya kupata habari, Haki na uhuru wa habari na vyombo vya habari na kadhalika.

URAIA

Wananchi wengi walipendekeza kuwa suala la Uraia libainishwe wazi kwenye Katiba. Tume imependekeza kwa kutaja Raia wa Jamhuri ya Muungano na haki zake.

MIKOPO NA DENI LA TAIFA

Ndugu Wananchi,
Wananchi walizungumzia suala la uwepo wa Ukomo wa nchi kukopa na uwepo wa utaratibu wa kulipa Deni la Taifa ili kuilinda Nchi isiwe na deni kubwa. Kwa kuzingatia maoni ya Wananchi, Tume imependekeza kuwa, Serikali itawajibika kutoa taarifa Bungeni kuhusu Mikopo kwa kuainisha kiasi cha deni lililopo, riba yake na matumizi ya fedha za Mikopo na utaratibu wa kulipa Madeni ya Taifa.

MFUMO WA UTAWALA

Kuhusu utawala, Tume inapendekeza Tanzania iendelee na mfumo wa Jamhuri kwa maana ya nchi inayoongozwa na Rais Mtendaji ambaye ni Mkuu wa nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu.

UCHAGUZI WA RAIS
Umri wa kugombea Urais

Tume ilipokea maoni yanayokinzana kuhusu umri wa mwananchi kugombea Urais. Baadhi walipendekeza mtu akishakuwa na sifa ya kupiga kura awe pia na sifa ya kugombea Urais. Umri wa mtu kuruhusiwa kupiga kura ni miaka 18. Wengine walipendekeza umri uliopo kwenye Katiba wa mtu kugombea Urais, yaani kuanzia miaka 40 na kuendelea, uendelee kubaki kama ulivyo.

Wengine walisema Umri wa mtu kuruhusiwa kugombea Urais uwe miaka 35 au miaka 50 na kuendelea.

Tume imeyachambua maoni yote hayo, ikafanya utafiti kwa kupitia Katiba za Nchi zingine na uhalisia wa watu wanaogombea na kuchaguliwa kuwa Marais katika Nchi mbalimbali Duniani ambazo zingine zimeruhusu wagombea wa nafasi ya Urais kuwa na umri chini ya miaka 40.

Wengi walioomba kugombea nafasi hiyo walikuwa na umri wa miaka 40 au zaidi.

Kwa kuzingatia maoni ya wananchi, utafiti na hali halisi, Tume inapendekeza Rais aendelea kuchaguliwa na wananchi na pamoja na sifa nyingine, mtu anayeomba urais asiwe chini ya miaka 40.

Uchaguzi wa Rais itakuwa kama ilivyo sasa, yaani mgombea Urais atakuwa na mgombea mwenza kwa utaratibu kama ilivyo sasa. Isipokuwa, Tume imependekeza Mgombea Urais anaweza kupendekezwa na Chama cha Siasa au kuwa Mgombea Huru.

Mgombea wa nafasi ya Rais atatangazwa kuwa mshindi iwapo atakuwa amepata kura zaidi ya asilimia hamsini ya kura zote zilizopigwa.

Hata hivyo, matokeo ya uchaguzi wa Rais yanaweza kulalamikiwa Mahakamani, lakini siyo kila mtu anaweza kufungua kesi. Wanaoweza kufungua kesi ni wagombea Urais. Aidha, ni Mahakama ya Juu pekee ndiyo itakuwa na Mamlaka na uwezo wa kusikiliza malalamiko kuhusu matokeo ya uchaguzi wa Rais na shauri lazima liamuliwe ndani ya mwezi mmoja, yaani siku therathini.

Rais aliyeshinda ataapishwa siku thelathini tangu alipotangazwa kuwa mshindi au kuthibitishwa na Mahakama.

MADARAKA YA RAIS

Ndugu Wananchi,
Tume inapendekeza kwamba, Rais abaki na madaraka ya uteuzi wa viongozi wa ngazi za juu. Hata hivyo inapendekezwa Rais ashirikiane na taasisi na vyombo vingine katika uteuzi. Kwa mfano:

Uteuzi wa Mawaziri na Manaibu Waziri, Rais atateua na Bunge litathibitisha.

Kuhusu Jaji Mkuu na Naibu Jaji Mkuu Rais atawateua kutokana na majina ya watu waliopendekezwa na Tume ya Uutumishi wa Mahakama na baada ya hapo Bunge litathibitisha.

Kuhusu Wakuu wa vyombo vya Ulinzi na Usalama inapendekezwa kianzishwe chombo kipya kitakachoitwa Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa, ambalo kati ya majukumu yake itakuwa ni kumshauri Rais kuhusu uteuzi wa Wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Kuhusu Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu watateuliwa na Rais kutokana na mapendekezo ya Tume ya Utumishi wa Umma.

KINGA YA RAIS

Tume baada ya kupitia maoni ya Wananchi, inapendekeza Rais abaki na kinga kama ilivyo sasa na anaweza kushitakiwa na Bunge kama ilivyo Katiba ya sasa.

IDADI YA MAWAZIRI

Inapendekezwa Rais aunde Serikali ndogo iliyo na Mawaziri wasiozidi kumi na tano na mawaziri hao wasiwe wabunge. Mawaziri hawatahudhuria vikao vya Bunge isipokuwa kama watahitajika kutoa ufafanuzi kwenye kamati za Bunge.

BUNGE

Ndugu Wananchi,
Kuhusu Bunge kutakuwa na wabunge wa aina mbili. Kutakuwa na Wabunge wa kuchaguliwa na wabunge watano wa kuteuliwa na Rais kuwakilisha Watu wenye Ulemavu.

Kila Jimbo la Uchaguzi litakuwa na Wabunge Wawili mmoja mwanamke na mwingine mwanamume.

Tume inapendekeza kwamba, Mbunge akifukuzwa na Chama cha Siasa abaki kuwa Mbunge lakini akihama Chama atapoteza Ubunge wake.

Inapendekezwa ukomo wa Ubunge uwe vipindi vitatu vya miaka mitano mitano. Hata hivyo, wananchi wanaweza kumwondoa mbunge wao kabla ya mwisho wa kipindi chake.

Inapendekezwa pia kusiwepo na uchaguzi mdogo isipokuwa kama nafasi inayokuwa wazi inatokana na Mbunge huru ndipo utafanyika uchaguzi mdogo kujaza nafasi hiyo, lakini kama nafasi ikiwa wazi kutokana na Mbunge wa Chama cha Siasa basi nafasi hiyo, ijazwe na mtu kutoka Chama hicho.

Inapendekezwa Spika na Naibu Spika wasitokane na Wabunge na wasiwe Viongozi wa vyama vya Siasa.

TUME YA UCHAGUZI

Tume imefanya uchambuzi wa maoni ya wananchi kuhusu Tume ya Uchaguzi. Tume inapendekeza jina la tume liwe Tume Huru ya Uchaguzi. Tume pia inapendekeza sifa za wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ziwekwe kwenye Katiba. Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi watapatikana kutoka miongoni mwa watu wenye sifa zilizoainishwa ndani ya Katiba kwa kuomba. Majina ya waombaji yatachambuliwa na Kamati ya Uteuzi ambayo Mwenyekiti wake atakuwa Jaji Mkuu na wajumbe wengine sita ambao ni Majaji Wakuu wa nchi Washirika, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Maspika wa Mabunge wa nchi Washirika na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu.

Kamati ya uteuzi itapendekeza majina ya watu wanaofaa kwa Rais ambaye atateua Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wengine. Bunge litathibitisha uteuzi wao. Wabunge na viongozi wa aina hiyo hawatakuwa na sifa za kuwa wajumbe wa tume ya uchaguzi.

Inapendekezwa Tume huru ya Uchaguzi isimamie masuala ya uchaguzi, kura ya maoni na Usajili wa Vyama vya Siasa.

MAHAKAMA

Kuhusu Mahakama inapendekezwa kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu (Supreme Court) Majaji wa Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani watateuliwa na Rais baada ya kupendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.

MUUNDO WA MUUNGANO

Ndugu Wananchi,
Suala la muundo wa Muungano ndilo lililokuwa gumu kuliko masuala yote. Tume ilitumia muda mwingi kuchambua maoni ya wananchi. Pamoja na kwamba hadidu za rejea zilielekeza Tume kuzingatia uwepo wa Muungano, baadhi ya wananchi walitoa maoni kwamba Muungano uvunjwe na Tume iliyapokea maoni hayo. Licha ya kwamba waliotaka kuvunjwa muungano walikuwa wachache sana, Tume ilichambua sababu walizotoa na kuridhika kwamba hazikuwa na uzito.

Wananchi walio wengi walitaka Muungano uendelee. Kati yao wapo waliopendekeza Muungano wa Serikali moja, Serikali mbili, Serikali tatu, Serikali nne na muungano wa mkataba. Sababu za wale waliopendekeza Serikali nne hazikuwa na uzito, kwa hiyo Tume ikaamua kutopendekeza muundo huo.

Wananchi waliopendekeza Serikali moja walikuwa wachache lakini sababu zao zilkuwa na uzito. Hata hivyo, Tume kwa kuzingatia hali halisi iliona ni changamoto kubwa kuwa na Muungano wa Serikali Moja.

Wananchi waliopendekeza Muungano wa Mkataba walikuwa wengi (hasa wananchi wa Zanzibar) na sababu zao zilikuwa na uzito. Lakini uchambuzi wa Tume ilionekana wazi kwamba ili kupata mkataba lazima kwanza kuwe na nchi mbili huru kabisa lakini hakukuwa na mazingira ya uhakika ya kupata mkataba wa muungano. Tume iliona kuna changamoto ya muungano kuvunjika ingawa waliotoa maoni walisisitiza muungano ubaki. Hivyo, Tume iliamua kutopendekeza muundo huo.

Wananchi waliopendekeza Tanzania iendelee na Muundo wa sasa wa Serikali mbili walikuwa wengi na sababu zao zilikuwa nzito. Hata hivyo, wananchi katika kundi hili walipendekeza mabadiliko mengi na makubwa. Tathmini ya Tume ilionyesha kwamba isingewezekana kufanya mabadiliko yote yaliyopendekezwa.

Wananchi waliopendekeza muundo wa Serikali tatu walikuwa wengi kuliko makundi yote. Sababu zao zilikuwa nzito lakini pia kulikuwa na changamoto nyingi na nzito. Pamoja na maoni ya wananchi Tume ilirejea sababu za kupendekeza muundo huu zilizotolewa na Tume zilizopita na Tafiti zilizofanywa na Tume kuhusu aina mbalimbali za Muungano. Baada ya yote hayo Tume ilifikia uamuzi wa kupendekeza mfumo wa Serikali tatu. Yaani Serikali ya Shirikisho, Serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

ORODHA YA MAMBO YA MUUNGANO

Ndugu Wananchi,
Tume imependekeza katika Rasimu ya Katiba kuwa orodha ya Mambo ya Muungano yawe 7 badala ya 22 yaliyopo sasa.
Mambo ya muungano yanayopendekwa ni:

Katiba na Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Uraia na Uhamiaji
Sarafu na Benki Kuu
Mambo ya Nje
Usajili wa Vyama vya Siasa
Ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo ya Kodi yatokanayo na Mambo ya Muungano.

BENKI KUU

Kwa kuwa Tume imependekeza Muungano wa Shirikisho kutokana na uzito wa maoni ya wananchi. Hivyokutakuwa na Benki Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakayokuwa na wajibu wa kusimamia masuala ya Sarafu na Fedha za Kigeni na Benki za Washirika wa Muungano.

BENKI ZA SERIKALI ZA WASHIRIKA

Kutokana na pendekezo la kuwepo kwa Serikali ya Shirikisho la Nchi tatu, inapendekezwa kuwepo kwa Benki zitakazokuwa na jukumu la kutunza akaunti ya fedha za Serikali za kila Mshirika wa Muungano na kuzisimamia benki za biashara katika mamlaka zao.

BAADHI YA MAMBO AMBAYO HAYAMO KWENYE RASIMU YA KATIBA
Serikali ya Majimbo

Ndugu Wananchi,
Tume ilipokea maoni kuhusu mambo mengine muhimu ambayo hayamo katika rasimu hii. Moja ya mambo hayo ni Serikali za Majimbo. Tume ilichambua maoni na sababu za wananchi kupendekeza Serikali za Majimbo lakini Tume ilibaini changamoto nyingi na ikaamua kutopendekeza muundo huu.

Kwanza, baada ya kuamua kupendekeza Muundo wa Muungano wa Serikali Tatu, ilionekana ni dhahiri kuongeza ngazi nyingine ya Serikali ingeleta gharama kubwa. Serikali nyingine kumi zingekuwa na Wakuu wa Majimbo, Mabaraza ya Mawaziri na Mabunge na gharama yake ingekuwa kubwa.

Pili, katika kutembelea nchi Tume ilishuhudia dalili za wazi za mivutano ya Udini, ukanda,malalamiko ya upendeleo wa baadhi ya maeneo na ukabila. Dalili zilikuwa wazi kwamba utawala wa majimbo ungeirudisha nchi kwenye utawala utakaoigawa nchi kwa misingi ya ukabila, udini na ukanda na kuzigawa rasilimali za taifa kikanda na hivyo kuleta tofauti kubwa ya kimaendeleo katika nchi.

Mahakama ya Kadhi

Ndugu wananchi,
Jambo la pili ni mahakama ya kadhi. Tume ilipokea maoni mengi kuhusu suala hili. Baadhi ya wananchi walitaka mahakama ya kadhi iingizwe kwenye Katiba na wengine walipinga. Baada ya kuamua kuwa Muundo wa Muungano uwe wa Serikali Tatu, Tume iliona kuwa Mahakama ya Kadhi siyo suala la Muungano na imeliacha ili lishughulikiwe na Washirika wa Muungano.
Hata hivyo ilionekana kuwa suala siyo kuwapo au kutokuwapo kwa mahakama ya kadhi. Mahakama hizo zinaweza kuwapo bila ya kuwa katika Katiba. Zanzibar kuna mahakama ya kadhi bila kuingizwa kwenye Katiba ya Zanzibar. Kwa kutumia uzoefu huo hata Tanzania Bara inaweza kupata ufumbuzi wa suala hili.

Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya

Jambo la Tatu ni Kuwepo au kutokuwepo kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya. Baadhi ya Wananchi walitaka Wakuu wa Mikoa na Wilaya wasiwepo, wengine walitaka Wakuu wa Mikoa na Wilaya waendelee kuwepo lakini wachaguliwe na wananchi na waengine wakasema wawepo na waendelee kuteuliwa na Rais kama ilivyo sasa. Tume ilitafakari kuhusu suala hili na kuamua kwamba siyo suala la Muungano na kwa kuwa Muundo wa Muungano imependekezwa uwe wa Serikali Tatu, Tume iliona suala la uwepo au kutokuwepo na namna ya upatikanaji wa Wakuu wa Mikoa na Wilaya lishughulikiwe na Washirika wa Muungano.

Serikali za Mitaa

Kuhusu Serikali za Mitaa, Tume ilipokea maoni kutoka kwa wananchi kuhusu kuziimarisha Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuzipatia uhuru kamili wa kujiamulia mambo yao bila kuingiliwa na Serikali Kuu. Tume ilitafakari suala hili na kuamua kwamba siyo jambo la Muungano na hivyo, litashughulikiwa kwenye Katiba za Washirika wa Muungano.

Uraia wa Nchi mbili

Ndugu Wananchi,
Jambo la tatu ni Uraia wa Nchi mbili. Tume ilipokea maoni kutoka kwa wananchi mbalimbali kuhusu kuwekwa kwenye Katiba suala la Uraia wa nchi mbili. Baada ya kufanya uchambuzi kwa kutengenisha mambo yapi ni ya Kikatiba na yapi yanaweza kutekelezwa bila kuingizwa kwenye Katiba bali kwenye Sheria inayohusu jambo husika, Tume imependekeza kuwa suala la Uraia wa nchi mbili linaweza kuwekwa kwenye Sheria badala ya kuwekwa kwenye Katiba. hii ni kwa sababu kutokana na utafiti uliofanywa na Tume, suala hilo linaweza kubadilika wakati wowote na hivyo likiwa kwenye Katiba linaweza kuifanya Katiba kubadilishwa mara kwa mara.

MWISHO

Naomba nichukue fursa hii kwa niaba ya Tume kuwashukuru Watanzania wote kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Mabadiliko ya Katiba, kuanzia hatua ya kutoa maoni na kuwachagua wawakilishi wenu watakaopata fursa ya kuipitia, kuijadili na kuitolea maoni Rasimu ya Katiba. Ushirikiano huu ulikuwa muhimu sana kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba hasa ukizingatia kuwa lengo ni kupata Katiba Mpya ambayo itaakisi ndoto na matakwa ya Wananchi wa Tanzania.

Tume ya Mabadiliko ya Katiba, inatoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar:

Kwa kuipatia vifaa afisi na mahitaji ya lazima
Kwa kuiwezesha Tume kutekeleza majukumu yake kwa ukamilifu,
Kwa kutokuingilia Uhuru wa Tume wakati wa Utekelezaji wa Majukumu yake na
Kutoa Wataalam wenye Weledi, Mahiri, Makini na Waadilifu ambao wameunda Sekretarieti ya Tume.

Ndugu Wananchi,
Shukrani za pekee ziwaendee:

Wakuu wa Mikoa,
Wakuu wa Wilaya,
Wakurugenzi / Makatibu wa Mamlaka za Serikali za Mitaa,
Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Wilaya,
Watendaji wa Kata, Vijiji, Mitaa na Masheha.

Kwa kuisaidia Tume kutekeleza Majukumu yake kwa ufanisi. Aidha, tunazishukuru Asasi za Kiraia, Taasisi, Jumuiya za Kidini, Vyama vya Siasa na Makundi mbalimbali kwa namna walivyoshiriki katika kuhamasisha wananchi kushiriki katika kutoa maoni.

Mwisho ingawa siyo kwa umuhimu, Tunawashukuru Wanahabari wote kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kuisaidia Tume kufikisha taarifa mbalimbali za Tume kwa Wananchi na katika kuhamasisha Wananchi kushiriki katika mchakato wa Mabadiliko ya Katiba.

Nachukua nafasi hii kuwaomba Wananchi kupitia Mabaraza ya Katiba ya Wilaya, Mabaraza ya Katiba ya Asasi, Taasisi na Makundi ya Watu wenye Malengo yanyofanana kushiriki vyema, kwa umakini, utulivu na kwa amani katika hatua hii ya kuipitia, kuijadili na kuitolea maoni Rasimu ya Katiba.

Tume imekuwa ikithamini na itandelea kuthamini mawazo na maoni kutoka kwa Watanzania wote.

Rasimu ya Katiba itapatikana kwenye tovuti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya
http://www.katiba.go.tz

SASA NAKUOMBA MHESHIMIWA MAKAMU WA RAIS UIZINDUE RASMI RASIMU YA KATIBA

Ahsanteni kwa kunisikiliza.

TOA MAONI TUPATE KATIBA MPYA

Saturday, June 1, 2013

Kigogo CUF mbaroni kwa vurugu za Mtwara

Jeshi la Polisi nchini linadaiwa kumkamata Mwenyekiti wa Jumuiya ya Vijana wa Chama cha CUF, Katani Ahmed Katani jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za uchochezi na kumsafirisha kwa ndege kwenda mkoani Mtwara.
Habari zilizolifikia Mwananchi Jumamosi na kuthibitishwa na Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro zilieleza kuwa Katani alikamatwa juzi mchana baada ya kupigiwa simu na maofisa wa polisi wa Kituo Kikuu cha Polisi jijini humo.
 
Hata hivyo Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alipoulizwa juu ya kukamatwa kwa kiongozi huyo alisema hana taarifa huku akiomba apewe muda ili aulize.
“Sina taarifa ngoja niulize”, alisema kwa kifupi na hata alipotafutwa baadaye hakupokea simu yake ya mkononi.
“Alipigiwa simu juzi na maofisa wa polisi na kuelezwa kuwa anahitajika kituoni hapo, lakini alipofika alikamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi” zilieleza habari hizo na kuongeza;

“Alihojiwa kwa saa kadhaa na jana asubuhi alisafirishwa kwa ndege kupelekwa mkoani Mtwara. Walitaka kumsafirisha kwa basi lakini viongozi wa CUF walikataa jambo hilo, hivyo kulazimika kusafirishwa kwa ndege.”

Habari hizo zilifafanua kwamba kwamba sababu kubwa ya kukamatwa kwa Katani ni kuhusishwa na vurugu zilizotokea mkoani Mtwara kati ya wananchi wanaopinga mradi wa bomba la gesi kutoka mkoani humo kwenda Dar es Salaam dhidi ya polisi.

Kwa upande wake Mtatiro alisema kuwa CUF hivi sasa inajipanga kuweka mawakili kabambe kwa ajili ya kumtetea kiongozi huyo wa vijana wa chama hicho.

“Tulijua tu kuna kiongozi wa chama atakamatwa maana kwa muda mrefu Polisi wamekuwa wakisema kuwa watawakamata viongozi wa juu wa chama. Kwa sasa Katani yupo Mtwara na sababu ya kukamatwa kwake ni kutuhumiwa kuchochea vurugu za Mtwara” alisema Mtatiro.

source: mwananchi


Thursday, May 30, 2013

Kinachodaiwa kumuua Msanii Mangwea hiki hapa

 
Dar es Salaam. Wakati mazishi ya mwanamuziki marehemu Albert Mangwea(28) maarufu kama `Ngwair’ yakitarajiwa kufanyika mjini Morogoro, maeneo ya Kihonda baada ya mwili kuwasili nchini, hospitali iliyomfanyia vipimo imethibitisha kuwa pombe na dawa za kulevya kupita kiasi ndivyo vilivyomuua.
Mwili wa mwanamuziki huyo, ambaye alitamba kwenye miaka ya 2000 na wimbo wa `Mikasi’, unatazamiwa kuletwa kesho nchini na kuagwa Jumamosi kabla ya kusafirishwa kwenda kwao Kihonda, Morogoro kwa mazishi.
Kwa mujibu wa taarifa Mangwea alifariki dunia juzi kwenye Hospitali ya St Hellen, iliyopo Johannesburg, Afrika Kusini alikokuwa amekwenda kwa shughuli za muziki.
 
Kifo chake
Ripoti iliyochapwa na mitandao mbalimbali ya ndani na nje ya nchi inasema marehemu alifikwa na umauti baada ya kulewa kupindukia, kibaya zaidi alikuwa hajala.
Siku ya kifo chake, Mangwea alianguka nyumbani kwa rafiki zake akiwa katika hali hiyo ya kulewa sana.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, baada ya kufikishwa hospitalini, Mangwea aligundulika kulewa mara tano ya kipimo cha kilevi kilichopitishwa na serikali ya Afrika ya Kusini, ambacho ni 416mg za pombe kwenye kila milimita 100(kwa mlevi anayeendesha chombo cha moto).
Pia marehemu alikutwa na upungufu wa hewa ya oksijeni kwenye seli na tishu za mwili wake.

Ripoti hiyo ilibainisha kuwa Mangwea, maarufu Ngwair, alikuwa na tatizo la kutokula chakula vizuri kabla ya kifo chake na pia kukosa muda wa kupumzika.

Sampuli zilizopatikana mwilini mwake zinaonyesha mkusanyiko wa dawa za kulevya mbalimbali zikiwemo heroine, cocaine chafu na bangi ya gramu 0.08 ambavyo vilikutwa kwenye damu yake.

Kifo chake kilitokana na mshtuko wa moyo na kushindwa kupumua, hali iliyosababisha mapigo ya moyo wake kusimama kwa sekunde chache, na kusababisha kifo chake.

Mwili wa Ngwair ulionekana kana kwamba alitokwa na damu nyingi puani baada ya kuonyeshwa kwa Watanzania wengi jana jioni Johannesburg, Afrika Kusini.

Taarifa za awali zilizotolewa na rafiki wa karibu aliyepo nchini Afrika Kusini, aliyejitambulisha kwa
 jina moja tu la Jonathan zilidai kuwa marehemu hakuamka tangu alipopumzika usiku wa kuamkia juzi.

Endelea: Mwananchi