Pages

Wednesday, July 31, 2013

Mambo ya kuangalia katika kuanzisha Mradi


Habari wanablog:

Hakika kwa yeyote anayetaka kuanzisha biashara yampasa kuwa makini na aina ya biashara anayotaka kuanzisha. Kumbuka lengo la kuanzisha biashara (mradi) ni kujipatia faida ama kuhakikisha mteja anaridhika na kile anachokipata. Kuna mambo ya msingi kadhaa ambayo mjasiriamali anaweza kutumia kama muongozo katika kuanzisha mradi mpya.

Uainishaji wa Fursa (opportunity identification)

Kabla hujaanzisha mradi jambo la muhimu na la msingi ni kuainisha fursa zilizopo katika eneo linalokuzunguka. Fursa ni mazingira chanya na saidizi ambayo mjasiriamali anatumia kuanzisha mradi na kujipatia faida nyingi kwa muda mfupi ama mrefu. Mara tu mjasiriamali anapotambua fursa zilizopo na kuamua kuanzisha mradi, akijua kuwa matarajio ya mradi huo ni chanya basi mjasiriamali huyo uwekezaji wake una matarajio yafuatayo.
  • Mradi kuwa na mapato mazuri na endelevu
  • Mradi kuwa na soko la uhakika
  • Gharama za uendeshaji wa mradi kuwa nafuu
  • Mradi kuwa na uwezekano wa kukua.
Utakapojiridhisha kuwa hayo ya juu yanaweza kudhihiri, basi unaweza kuwekeza na kuanzisha mradi wa bidhaa ama utoaji huduma, kwa sababu kuna uwezekano mkubwa wa upatikanaji wa faida.
 
Vyanzo vya utambuzi wa fursa
 
  • Mabadiliko ya teknolojia- hapa tumeona jinsi makundi mbalimbali yalivyofaidika na mabadilikoya teknolojia..Mfano watu wamejiajiri kupitia huduma za simu na kujipatia faida kupitia M-pesa, Tigo-pesa, Airtel money.....zamani fursa hizi hazikuepo. Pia kuna blogs za kibiashara mbali mbali zimeanzishwa nia na lengo ni kujipatia kipato kupitia kwa wadhamini: Mfano Mjengwa blog, Michuzi blog na jamii forum. Bado hujachelewa fursa zinazopatikana juu ya mabadiliko ya teknolojia zipo nyingi na kwenye sekta tofauti tofauti.
 
  • Uelewa- Kwenye jamii yoyote uelewa wa mambo unapoongezeka huambatana na fursa mbali mbali za kiuchumi zinazoendana na kuongezeka kwa uelewa. Mathani mahitaji ya vyakula vilivyo salama na kemikali umekuwa mkubwa, kulinganisha na vyakula vinavyotokana na kemikali, hii ina sababishwa na watu kuwa na elimu juu ya madhara ya kemikali mwilini.
 
  • Mabadiliko ya sera-
Itaendelea: Niandikie mmlanzi@yahoo.com
 

Monday, July 29, 2013

Mradi ama biashara (Enterprise)


Habari wana blog:

Leo tunaendelea na mada yetu ya ujasiriamali baada ya kuwa katika mapumziko ya mwisho wa wiki, kwa kujifunza nadharia ya mambo mbalimbali yanayopatikana kwenye ujasiriamali. Chapisho la mwisho tuliona sifa mbali mbali za mjasiriamali kinadharia. Leo hii tunaenda kuangalia biashara ama miradi ambayo mjasiriamali anaweza kijishughulisha nayo ili aweze kutimiza lengo lake lake la kujipatia faida na kumridhisha mteja. Kumbuka huwezi fanya jambo lolote kwa ufasaha zaidi kama hujui nadharia ya jambo hilo kwa ufasaha zaidi.
 
Mradi/Miradi ni nini?
Kwa lugha ya kijasiriamali Mradi ni biashara unayoitekeleza (commercial untertaking) ima kuzalisha bidhaa ama kutoa huduma kwa lengo la la kujipatia faida na kuridhisha wateja. Takwimu zinaonesha kuwa asilimia kubwa ya watanzania wanajishughulisha na kilimo. Kilimo hapa ni neno pana kwa maana ya uzalishaji wa mazao mfano: Mahindi, Mpunga (Mchele), viazi na mazao mengine mbali mbali unayoyafahamu, matunda, mbogamboga na maua.
 
Pia kilimo kinahusu ufugaji wa wanyama mbali mbali mfano: Ng'ombe, Mbuzi, Nguruwe na Kondoo:Ufugaji wa ndege Mfano: Kuku, bata, njiwa na kanga. Ufugaji huwa na lengo la uzalishaji wa bidhaa kama nyama, ngozi, maziwa, mayai na bidhaa nyingine zitokanazo na wanyama ama ndege.
 
Kwa hiyo mradi unaweza kuwa ni uzalishaji wa bidhaa kama tulivyoona hapo juu, pia mradi unaweza kujikita kwenye utoaji huduma. Mathalani afisa ugani ambaye ana taaluma ya utabibu wa mifugo anaweza kutibu mifugo kumi mpaka ishirini kwa siku na kulipwa ujira kwa kutoa huduma hiyo. Kuna huduma nyingi hutolewa na kisha ujira hutolewa baada ya huduma hiyo kupatikana. Mfano wa huduma hizo ni Ufundishaji (elimu), mawasiliano, ushauri, matengenezo, ufundi, usafirishaji , udalali n.k.
 
Somo tunaloweza kujifunza hapa ni kwamba mjasiriamali ana wigo mpana wa kuchagua aina ya mradi anaotaka kuutekeleza, aidha azlishe bidhaa ama atoe huduma. Miradi hii hutofautiana kulingana na mtaji uliowekezwa kwenye mradi husika na kufanya miradi hyo iwe ya aina mbili aidha midogo (micro enterprise) ama mikubwa (Macro enterprise).
 
 
Itaendelea: niandikie mmlanzi@yahoo.com
 
 

Friday, July 26, 2013

Mjasiriamali na Mfanyabiashara


Habari wana blog:

Chapisho la mwisho tuliona kwa ufupi na maana nyepesi ya neno ujasiriamali na kuangalia jinsi mjasiriamali anavyowezesha kutumia rasilimali ardhi, watu, maji na mtaji kuweza kufanya uzalishaji aidha wa mazao (bidhaa) ama kutoa huduma kwa lengo la kujipatia faida.
 
Ubunifu
Bado neno Mjasiriamali linaweza kuwa na maana nyingi ikiwemo ya uwezo wa mtu (mfanyabiashara) kubuni (innovations) kitu (vitu) vipya na kuvitambulisha katika jamii inayomzunguka katika jitihada ya kufanya vitu hivyo viwe na uwezo wa kujikwamua kiuchumi.
 
Kumbuka sio wafanyabiashara wote ni wajasiriamali, ila wajasiriamali wote ni wafanyabishara. Sifa mojawapo ya mjasiriamali ni kuwa mbunifu wa vitu vipya (bidhaa ama huduma). Huduma kama njia mojawapo ya kupata faida ni kama vile haifahamiki miongoni mwa watanzania wengi. Wengi wetu hufikiri ili uweze kupata kipato ni vyema ukauza bidhaa, huku utoaji wa huduma ukiachwa kwa watu wachache ambao hutumia fursa hiyo kupata faida kubwa.
 
Hivyo ubunifu huweza kusababisha biashara mpya kujitokeza na kuajiri ama kutumika kama ajira binafsi kwa msururu wa wafanyabishara wengine (duplication). Hapo juu tumeona kuwa si wafanyabiashara wote ni wajasiriamali, ila wajasirimali wote ni wafanyabiashara. Hii ni kwa sababu mjasiriamali ana sifa za ziada na za kipekee kumshinda mfanyabiashara.

Sifa hizi za ziada za mjasiriamali ni Mbunifu (innovator), kujitegemea (independent), kujiamini (self-confidence), mpangiliaji (organized), muono (vision), sugu (persistent), Tumaini (optimism), commited, mtendaji (action-oriented), mtatuzi wa matatizo (problem solver), kujihusisha na hatari: kutoogopa kupata hasara (risk taker) na anayenyumbulika (flexiblity).

Sifa hizi ni za mjasiriamali aliyekamilika na aghalabu kukuta mfanyabiashara kuwa nazo. Usihofu kama hauna kipaji cha ubunifu, unaweza kuiga mambo mazuri kutoka kwa wabunifu na ukayatumia ili uweze kujikwamua kuchumi.
 
Itaendelea
 
 Unaweza kukomenti kwenye hii blog :

 Ama niandikie maboresho kwenye mmlanzi@yahoo.com
 

Thursday, July 25, 2013

Ujasiriamali ni nini?

Wapenzi wa blog hii nimeamua kubadili mfumo wa blog hii kutoka katika kuleta taarifa mbali mbali za kijamii na kujikita zaidi na dhana nzima ya ujasirimali. Blog hii itakuwa inakuletea tips mbalimbali za ujasiriamali kwa kadiri ya uwezo utakavyokuwa unapatikana. Hivyo nategemea mafunzo mengi pia kutoka kwa wasomaji wa blog hii ili tuweze kuondoka katika mzunguko huu wa umasikini.
 
 Lengo kuu ni kusaidia watanzania wenzangu kujua mbinu mbalimbali zinazotumiwa na wafanyabiashara mbali mbali kupata mafanikio ya kibiashara, kutumia mbinu hizo kwa kuiga ama kuibua mbinu mbadala ili tuweze kuondokana na umaskini.
 
Huku idadi ya watu ikizidi kuongezeka duniani na Nchini kwetu kwa ujumla, changamoto kuu imekua suala la ajira. Kila mmoja wetu anataka kuajiriwa aidha serikalini ama kwenye sekta binafsi huku suala la kujiajiri likiwa la mwisho katika vipaumbele.
 
Ujasiriamali ni nini?
 
Kwa sasa ni jina maarufu sana hapa Tanzania, mtu yeyote aliyefanikiwa katika biashara hupewa jina hili. Maana ya ujasirimali inabaki katika uwezo wa kufanya maamuzi sahihi wa kutumia rasilimali chache zinazokuzunguka vizuri ili uweze kupata faida.
 
Mathalani rasilimali zinazokuzunguka ni ardhi, watu na maji, ni vipi mchanganyiko huu utautumia vizuri ili uweze kupata zao (output) ambayo itakusaidia kujikwamua katika hali uliyonayo. Ama ni vipi utatumia mtaji mdogo ulionao kufanya biashara itakayokuletea faida ambayo utaitumia kuongeza mtaji na kuikuza biashara yako.
 
Fahamu kwamba lengo lolote la mjasiriamali ni kupata faida na kumridhisha mteja ambaye anatumia bidhaa ama huduma inayotolewa na mjasiriamali. Bidhaa ama huduma ndio msingi wa mjasirimali yeyote ambaye anataka kupata faida. Mathalani mkulima wa mahindi bidhaa yake ni mahindi hivyo atauza mahindi kujipatia faida, na mtabibu wa mifugo anatoa huduma ya matibabu kwa mifugo na kulipwa ujira kwa kutoa huduma hiyo.
 
Itaendelea....
 
Niandikie: mmlanzi@yahoo.com
 
 

Tuesday, June 4, 2013

Full: Hotuba ya Mh Jaji Sinde Warioba: Uzinduzi wa Rasimu ya Katiba Mpya!

 
HOTUBA YA MWENYEKITI WA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA, JAJI JOSEPH S. WARIOBA, KATIKA MKUTANO WA WAANDISHI WA HABARI KUHUSU UZINDUZI WA RASIMU YA KATIBA TAREHE 03 JUNI, 2013 KWENYE VIWANJA VYA UKUMBI WA KARIMJEE,
DAR ES SALAAM
.
Mhe. Dkt Mohammed Gharib Bilali – Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano,
Mhe. Mizengo K. P. Pinda (Mb.) – Waziri Mkuu,
Mhe. Seif Sharif Hamad – Makamu wa Kwanza wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Mhe. Balozi Seif Ali Iddi (Mb.) – Makamo wa Pili wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Mhe. Mathias Chikawe – Waziri wa Katiba na Sheria,
Mhe. Abubakar Khamis Bakary – Waziri wa Katiba na Sheria wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Mhe. Jaji Frederick M Werema – Mwanasheria Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Othman Masoud Othuman – Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar,
Viongozi wa Vyama vya Siasa,
Waheshimiwa Wajumbe wa Tume na Wajumbe wa Sekretarieti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba,
Ndugu Wananchi,
Wageni Waalikwa
Waandishi wa Habari Mabibi na Mabwana.

UTANGULIZI

Ndugu Wananchi,
Awali ya yote namshukuru mwenyezi mungu kwa kutuwezesha kufikia hatua hii ya leo ya kuzindua Rasimu ya Katiba. pia, niwashukuru ninyi nyote mliohudhuria halfa hii ikiwa ni mwendelezo wa mchakato muhimu wa Mabadiliko ya Katiba ya nchi yetu.

Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilipitishwa Bungeni Novemba, 2011 na kufanyiwa mabadiliko Februari, 2012. Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliundwa kwa mujibu wa Kifungu 6(1) cha sheria hiyo (Cap.83). Wajumbe 34 wa Tume waliteuliwa na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, mwezi Aprili, 2012. Kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Tume imepewa miezi kumi na minane kukamilisha kazi yake kuanzia siku ilipoanza kazi rasmi ambayo ilikuwa Mei 2, 2012.

Tume iliandaa ratiba ya utekelezaji wa majukumu yake. Kufuatana na ratiba hiyo Tume ilijipanga kukusanya maoni ya wananchi katika kipindi cha miezi mitano kuanzia Mwezi Julai hadi Disemba, 2012. Kazi hiyo ilifanywa kama tulivyopanga. Tume ilijigawa katika makundi na ilitembelea mkoa yote thelathini.

Tume ilifanya mikutano 1,942 ambayo ilihudhuriwa na wananchi wapatao 1,365,337 ambao kati ya hao wananchi 333,537 walitoa maoni ama kwa mazungumzo ya ana kwa ana au kwa maandishi. Tume pia ilipata maoni ya wananchi wengi, wa ndani na nje ya nchi kwa njia mbali mbali kama vile; Mikutano ya hadhara, Fomu maalum za Tume, barua kupitia Masanduku ya Barua ya Tume, Mitandao ya Kijamii ya barua pepe; facebook ya Tume, Tovuti ya Tume; Makala mbalimbali kutoka kwenye magazeti na ujumbe mfupi wa simu.

Tume ilitumia mwezi Januari, 2013 kukusanya maoni ya makundi mbali mbali katika jamii, ikiwa ni pamoja na vyama vya siasa, taasisi za Serikali, taasisi za dini, wakulima, wafugaji, wafanyakazi, asasi za kiraia na kadhalika. Makundi zaidi ya 160 yalikutana na Tume na kutoa maoni. Tume pia ilipata maoni ya viongozi wa juu wa Serikali walioko madarakani na waliostaafu. Kwa jumla viongozi 43walitoa maoni.

Tume ilipanga kutumia miezi mitatu ya Februari, Machi na Aprili kuchambua maoni ya wananchi na kuandaa Rasimu ya Katiba. Lakini tuligundua kwamba maoni tuliyopata yalikuwa mengi sana, na pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa, tulitambua umuhimu wa kuongeza muda hadi mwisho wa mwezi Mei, Maoni ya wananchi yaligusa mambo yote yanayohusu Katiba na mengi ya maoni hayo yalikinzana. Aidha, baadhi ya maoni yaligusia masuala ya Kisera, Kisheria na Kiutendaji. Tulifanya uchambuzi makini na wa ndani wa maoni hayo na kazi hiyo tumeikamilisha na rasimu imeandaliwa na Tume na leo tupo hapa kwa ajili ya kuizindua, ambapo Wananchi watapata nafasi ya kuisoma. Kwa leo, kwa niaba ya Tume, napenda kutaja maeneo machache tu ambayo tunayapendekeza.

IBARA ZINAZOPENDEKEZWA KWENYE RASIMU YA KATIBA

Ndugu Wananchi,
Katiba yetu ya sasa ina ibara 152. Tume ilifanya jitihada kubwa sana kuandaa rasimu ambayo siyo ndefu. Lakini katika hali halisi haikuwezekana. Rasimu ya Katiba tunayopendekeza ina ibara 240.

MISINGI MIKUU YA TAIFA

Utangulizi wa Katiba ya sasa ndio unaobeba misingi mikuu ya Taifa ambayo ni Uhuru, Haki, Udugu na Amani. Tume inaamini kwamba misingi hii ni mizito na inastahili kubaki kwenye Katiba mpya. Hata hivyo, Tume imeona ni busara kuongeza misingi mingine mitatu ya Usawa, Umoja na Mshikamano. Hivyo, Tume imependekeza Katiba iwe na Misingi Mikuu saba ya Taifa;yaani; Uhuru, Haki, Udugu, Usawa, Umoja, Amani na Mshikamano.

TUNU ZA TAIFA

Katiba yetu ya sasa haina sehemu inayoelezea tunu za Taifa (National Values). Wananchi wengi walitoa maoni kwamba Katiba itaje Tunu za Taifa. Tume imependekeza Tunu zifuatazo zitajwe ndani ya Katiba. Tunu hizo ni;- Utu, Uzalendo, Uadilifu, Umoja, Uwazi, Uwajibikaji na Lugha yetu ya taifa ya Kiswahili.

MALENGO YA TAIFA

Tume ilipozunguka nchi nzima wananchi walizungumzia sana kuhusu malengo ya taifa. Walitaka Katiba ionyeshe dira ya taifa. Wananchi wanayo ndoto yao ya Tanzania ya kesho na kesho kutwa. Kwa kuzingatia maoni ya wananchi, kuna sura nzima inayohusu Malengo mahsusi na ya msingi ya mwelekeo wa shughuli za Kiserikali na Sera za Kitaifa. Rasimu ya Katiba inaeleza kuwa Malengo ya Kitaifa yaliyoainishwa ndani ya Rasimu yatakuwa ni Mwongozo kwa Serikali, Bunge, Mahakama, Vyama vya Siasa, Taasisi na Mamlaka nyingine, na kwa kila mwananchi katika matumizi au kutafsiri Masharti ya Katiba au Sheria nyingine za Nchi.
Kwa msingi huo, Tume imependekeza malengo makuu ya taifa yapanuliwe kwa mpangilio wa kuonesha malengo ya kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutamaduni, kimazingira na sera ya mambo ya nje. Malengo hayo yameingizwa kwenye Rasimu ya Katiba.

VYOMBO VYA KIKATIBA

Wananchi walizungumzia suala la kubainishwa kwa vyombo vya Kikatiba na kuingizwa kwenye Katiba ili viwe na nguvu ya Kikatiba katika utekelezaji wa majukumu yao. Tume imependekeza baadhi ya vyombo vifuatavyo viwe vya Kikatiba; Tume ya Uhusiano na Uratibu wa Serikali, Baraza la Mawaziri, Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu na Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri; Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa, Tume Huru ya Uchaguzi, Tume ya Utumishi wa Mahakama, Tume ya Utumishi wa Umma, Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora

MAADILI YA VIONGOZI NA MIIKO YA UONGOZI

Wananchi wengi pia walizungumzia kwa upana sana kuhusu maadili na miiko ya Viongozi, kwa kuzingatia maoni ya wananchi Tume inapendekeza maadili ya viongozi wa umma, pamoja na miiko ya uongozi yawekwe kwenye Katiba. Tume pia imependekeza kuwa Sekretariati ya Maadili ibadilishwe kuwa Tume yenye mamlaka makubwa ya kusimamia maadili ya viongozi wanaovunja miiko ya uongozi.

HAKI ZA BINADAMU

Kuhusu haki za binadamu wananchi walitaka haki hizi ziimarishwe na kusiwe na vikwazo visivyo vya lazima. Tume imependekeza mabadiliko katika baadhi ya haki za binadamu kwa madhumuni ya kuziimarisha. Moja ya mabadiliko hayo ni kuhusu uhuru wa mwananchi kushiriki shughuli za umma. Tume inapendekeza kwamba vikwazo vilivyowekwa kuzuia mgombea huru viondolewe. Kwa maana nyingine Tume inapendekeza mgombea binafsi aruhusiwe.

Tume pia, inapendekeza haki mpya ziingizwe kwenye Katiba ikiwa ni pamoja na haki ya wafanyakazi, , haki ya mtoto, haki za Watu wenye Ulemavu, Haki za Wanawake, Haki za Wazee, Haki za Makundi Madogo katika Jamii, Haki ya Elimu na Kujifunza, Haki ya kupata habari, Haki na uhuru wa habari na vyombo vya habari na kadhalika.

URAIA

Wananchi wengi walipendekeza kuwa suala la Uraia libainishwe wazi kwenye Katiba. Tume imependekeza kwa kutaja Raia wa Jamhuri ya Muungano na haki zake.

MIKOPO NA DENI LA TAIFA

Ndugu Wananchi,
Wananchi walizungumzia suala la uwepo wa Ukomo wa nchi kukopa na uwepo wa utaratibu wa kulipa Deni la Taifa ili kuilinda Nchi isiwe na deni kubwa. Kwa kuzingatia maoni ya Wananchi, Tume imependekeza kuwa, Serikali itawajibika kutoa taarifa Bungeni kuhusu Mikopo kwa kuainisha kiasi cha deni lililopo, riba yake na matumizi ya fedha za Mikopo na utaratibu wa kulipa Madeni ya Taifa.

MFUMO WA UTAWALA

Kuhusu utawala, Tume inapendekeza Tanzania iendelee na mfumo wa Jamhuri kwa maana ya nchi inayoongozwa na Rais Mtendaji ambaye ni Mkuu wa nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu.

UCHAGUZI WA RAIS
Umri wa kugombea Urais

Tume ilipokea maoni yanayokinzana kuhusu umri wa mwananchi kugombea Urais. Baadhi walipendekeza mtu akishakuwa na sifa ya kupiga kura awe pia na sifa ya kugombea Urais. Umri wa mtu kuruhusiwa kupiga kura ni miaka 18. Wengine walipendekeza umri uliopo kwenye Katiba wa mtu kugombea Urais, yaani kuanzia miaka 40 na kuendelea, uendelee kubaki kama ulivyo.

Wengine walisema Umri wa mtu kuruhusiwa kugombea Urais uwe miaka 35 au miaka 50 na kuendelea.

Tume imeyachambua maoni yote hayo, ikafanya utafiti kwa kupitia Katiba za Nchi zingine na uhalisia wa watu wanaogombea na kuchaguliwa kuwa Marais katika Nchi mbalimbali Duniani ambazo zingine zimeruhusu wagombea wa nafasi ya Urais kuwa na umri chini ya miaka 40.

Wengi walioomba kugombea nafasi hiyo walikuwa na umri wa miaka 40 au zaidi.

Kwa kuzingatia maoni ya wananchi, utafiti na hali halisi, Tume inapendekeza Rais aendelea kuchaguliwa na wananchi na pamoja na sifa nyingine, mtu anayeomba urais asiwe chini ya miaka 40.

Uchaguzi wa Rais itakuwa kama ilivyo sasa, yaani mgombea Urais atakuwa na mgombea mwenza kwa utaratibu kama ilivyo sasa. Isipokuwa, Tume imependekeza Mgombea Urais anaweza kupendekezwa na Chama cha Siasa au kuwa Mgombea Huru.

Mgombea wa nafasi ya Rais atatangazwa kuwa mshindi iwapo atakuwa amepata kura zaidi ya asilimia hamsini ya kura zote zilizopigwa.

Hata hivyo, matokeo ya uchaguzi wa Rais yanaweza kulalamikiwa Mahakamani, lakini siyo kila mtu anaweza kufungua kesi. Wanaoweza kufungua kesi ni wagombea Urais. Aidha, ni Mahakama ya Juu pekee ndiyo itakuwa na Mamlaka na uwezo wa kusikiliza malalamiko kuhusu matokeo ya uchaguzi wa Rais na shauri lazima liamuliwe ndani ya mwezi mmoja, yaani siku therathini.

Rais aliyeshinda ataapishwa siku thelathini tangu alipotangazwa kuwa mshindi au kuthibitishwa na Mahakama.

MADARAKA YA RAIS

Ndugu Wananchi,
Tume inapendekeza kwamba, Rais abaki na madaraka ya uteuzi wa viongozi wa ngazi za juu. Hata hivyo inapendekezwa Rais ashirikiane na taasisi na vyombo vingine katika uteuzi. Kwa mfano:

Uteuzi wa Mawaziri na Manaibu Waziri, Rais atateua na Bunge litathibitisha.

Kuhusu Jaji Mkuu na Naibu Jaji Mkuu Rais atawateua kutokana na majina ya watu waliopendekezwa na Tume ya Uutumishi wa Mahakama na baada ya hapo Bunge litathibitisha.

Kuhusu Wakuu wa vyombo vya Ulinzi na Usalama inapendekezwa kianzishwe chombo kipya kitakachoitwa Baraza la Ulinzi na Usalama la Taifa, ambalo kati ya majukumu yake itakuwa ni kumshauri Rais kuhusu uteuzi wa Wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Kuhusu Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu watateuliwa na Rais kutokana na mapendekezo ya Tume ya Utumishi wa Umma.

KINGA YA RAIS

Tume baada ya kupitia maoni ya Wananchi, inapendekeza Rais abaki na kinga kama ilivyo sasa na anaweza kushitakiwa na Bunge kama ilivyo Katiba ya sasa.

IDADI YA MAWAZIRI

Inapendekezwa Rais aunde Serikali ndogo iliyo na Mawaziri wasiozidi kumi na tano na mawaziri hao wasiwe wabunge. Mawaziri hawatahudhuria vikao vya Bunge isipokuwa kama watahitajika kutoa ufafanuzi kwenye kamati za Bunge.

BUNGE

Ndugu Wananchi,
Kuhusu Bunge kutakuwa na wabunge wa aina mbili. Kutakuwa na Wabunge wa kuchaguliwa na wabunge watano wa kuteuliwa na Rais kuwakilisha Watu wenye Ulemavu.

Kila Jimbo la Uchaguzi litakuwa na Wabunge Wawili mmoja mwanamke na mwingine mwanamume.

Tume inapendekeza kwamba, Mbunge akifukuzwa na Chama cha Siasa abaki kuwa Mbunge lakini akihama Chama atapoteza Ubunge wake.

Inapendekezwa ukomo wa Ubunge uwe vipindi vitatu vya miaka mitano mitano. Hata hivyo, wananchi wanaweza kumwondoa mbunge wao kabla ya mwisho wa kipindi chake.

Inapendekezwa pia kusiwepo na uchaguzi mdogo isipokuwa kama nafasi inayokuwa wazi inatokana na Mbunge huru ndipo utafanyika uchaguzi mdogo kujaza nafasi hiyo, lakini kama nafasi ikiwa wazi kutokana na Mbunge wa Chama cha Siasa basi nafasi hiyo, ijazwe na mtu kutoka Chama hicho.

Inapendekezwa Spika na Naibu Spika wasitokane na Wabunge na wasiwe Viongozi wa vyama vya Siasa.

TUME YA UCHAGUZI

Tume imefanya uchambuzi wa maoni ya wananchi kuhusu Tume ya Uchaguzi. Tume inapendekeza jina la tume liwe Tume Huru ya Uchaguzi. Tume pia inapendekeza sifa za wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ziwekwe kwenye Katiba. Wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi watapatikana kutoka miongoni mwa watu wenye sifa zilizoainishwa ndani ya Katiba kwa kuomba. Majina ya waombaji yatachambuliwa na Kamati ya Uteuzi ambayo Mwenyekiti wake atakuwa Jaji Mkuu na wajumbe wengine sita ambao ni Majaji Wakuu wa nchi Washirika, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Maspika wa Mabunge wa nchi Washirika na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu.

Kamati ya uteuzi itapendekeza majina ya watu wanaofaa kwa Rais ambaye atateua Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wengine. Bunge litathibitisha uteuzi wao. Wabunge na viongozi wa aina hiyo hawatakuwa na sifa za kuwa wajumbe wa tume ya uchaguzi.

Inapendekezwa Tume huru ya Uchaguzi isimamie masuala ya uchaguzi, kura ya maoni na Usajili wa Vyama vya Siasa.

MAHAKAMA

Kuhusu Mahakama inapendekezwa kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu (Supreme Court) Majaji wa Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani watateuliwa na Rais baada ya kupendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.

MUUNDO WA MUUNGANO

Ndugu Wananchi,
Suala la muundo wa Muungano ndilo lililokuwa gumu kuliko masuala yote. Tume ilitumia muda mwingi kuchambua maoni ya wananchi. Pamoja na kwamba hadidu za rejea zilielekeza Tume kuzingatia uwepo wa Muungano, baadhi ya wananchi walitoa maoni kwamba Muungano uvunjwe na Tume iliyapokea maoni hayo. Licha ya kwamba waliotaka kuvunjwa muungano walikuwa wachache sana, Tume ilichambua sababu walizotoa na kuridhika kwamba hazikuwa na uzito.

Wananchi walio wengi walitaka Muungano uendelee. Kati yao wapo waliopendekeza Muungano wa Serikali moja, Serikali mbili, Serikali tatu, Serikali nne na muungano wa mkataba. Sababu za wale waliopendekeza Serikali nne hazikuwa na uzito, kwa hiyo Tume ikaamua kutopendekeza muundo huo.

Wananchi waliopendekeza Serikali moja walikuwa wachache lakini sababu zao zilkuwa na uzito. Hata hivyo, Tume kwa kuzingatia hali halisi iliona ni changamoto kubwa kuwa na Muungano wa Serikali Moja.

Wananchi waliopendekeza Muungano wa Mkataba walikuwa wengi (hasa wananchi wa Zanzibar) na sababu zao zilikuwa na uzito. Lakini uchambuzi wa Tume ilionekana wazi kwamba ili kupata mkataba lazima kwanza kuwe na nchi mbili huru kabisa lakini hakukuwa na mazingira ya uhakika ya kupata mkataba wa muungano. Tume iliona kuna changamoto ya muungano kuvunjika ingawa waliotoa maoni walisisitiza muungano ubaki. Hivyo, Tume iliamua kutopendekeza muundo huo.

Wananchi waliopendekeza Tanzania iendelee na Muundo wa sasa wa Serikali mbili walikuwa wengi na sababu zao zilikuwa nzito. Hata hivyo, wananchi katika kundi hili walipendekeza mabadiliko mengi na makubwa. Tathmini ya Tume ilionyesha kwamba isingewezekana kufanya mabadiliko yote yaliyopendekezwa.

Wananchi waliopendekeza muundo wa Serikali tatu walikuwa wengi kuliko makundi yote. Sababu zao zilikuwa nzito lakini pia kulikuwa na changamoto nyingi na nzito. Pamoja na maoni ya wananchi Tume ilirejea sababu za kupendekeza muundo huu zilizotolewa na Tume zilizopita na Tafiti zilizofanywa na Tume kuhusu aina mbalimbali za Muungano. Baada ya yote hayo Tume ilifikia uamuzi wa kupendekeza mfumo wa Serikali tatu. Yaani Serikali ya Shirikisho, Serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

ORODHA YA MAMBO YA MUUNGANO

Ndugu Wananchi,
Tume imependekeza katika Rasimu ya Katiba kuwa orodha ya Mambo ya Muungano yawe 7 badala ya 22 yaliyopo sasa.
Mambo ya muungano yanayopendekwa ni:

Katiba na Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Uraia na Uhamiaji
Sarafu na Benki Kuu
Mambo ya Nje
Usajili wa Vyama vya Siasa
Ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo ya Kodi yatokanayo na Mambo ya Muungano.

BENKI KUU

Kwa kuwa Tume imependekeza Muungano wa Shirikisho kutokana na uzito wa maoni ya wananchi. Hivyokutakuwa na Benki Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakayokuwa na wajibu wa kusimamia masuala ya Sarafu na Fedha za Kigeni na Benki za Washirika wa Muungano.

BENKI ZA SERIKALI ZA WASHIRIKA

Kutokana na pendekezo la kuwepo kwa Serikali ya Shirikisho la Nchi tatu, inapendekezwa kuwepo kwa Benki zitakazokuwa na jukumu la kutunza akaunti ya fedha za Serikali za kila Mshirika wa Muungano na kuzisimamia benki za biashara katika mamlaka zao.

BAADHI YA MAMBO AMBAYO HAYAMO KWENYE RASIMU YA KATIBA
Serikali ya Majimbo

Ndugu Wananchi,
Tume ilipokea maoni kuhusu mambo mengine muhimu ambayo hayamo katika rasimu hii. Moja ya mambo hayo ni Serikali za Majimbo. Tume ilichambua maoni na sababu za wananchi kupendekeza Serikali za Majimbo lakini Tume ilibaini changamoto nyingi na ikaamua kutopendekeza muundo huu.

Kwanza, baada ya kuamua kupendekeza Muundo wa Muungano wa Serikali Tatu, ilionekana ni dhahiri kuongeza ngazi nyingine ya Serikali ingeleta gharama kubwa. Serikali nyingine kumi zingekuwa na Wakuu wa Majimbo, Mabaraza ya Mawaziri na Mabunge na gharama yake ingekuwa kubwa.

Pili, katika kutembelea nchi Tume ilishuhudia dalili za wazi za mivutano ya Udini, ukanda,malalamiko ya upendeleo wa baadhi ya maeneo na ukabila. Dalili zilikuwa wazi kwamba utawala wa majimbo ungeirudisha nchi kwenye utawala utakaoigawa nchi kwa misingi ya ukabila, udini na ukanda na kuzigawa rasilimali za taifa kikanda na hivyo kuleta tofauti kubwa ya kimaendeleo katika nchi.

Mahakama ya Kadhi

Ndugu wananchi,
Jambo la pili ni mahakama ya kadhi. Tume ilipokea maoni mengi kuhusu suala hili. Baadhi ya wananchi walitaka mahakama ya kadhi iingizwe kwenye Katiba na wengine walipinga. Baada ya kuamua kuwa Muundo wa Muungano uwe wa Serikali Tatu, Tume iliona kuwa Mahakama ya Kadhi siyo suala la Muungano na imeliacha ili lishughulikiwe na Washirika wa Muungano.
Hata hivyo ilionekana kuwa suala siyo kuwapo au kutokuwapo kwa mahakama ya kadhi. Mahakama hizo zinaweza kuwapo bila ya kuwa katika Katiba. Zanzibar kuna mahakama ya kadhi bila kuingizwa kwenye Katiba ya Zanzibar. Kwa kutumia uzoefu huo hata Tanzania Bara inaweza kupata ufumbuzi wa suala hili.

Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya

Jambo la Tatu ni Kuwepo au kutokuwepo kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya. Baadhi ya Wananchi walitaka Wakuu wa Mikoa na Wilaya wasiwepo, wengine walitaka Wakuu wa Mikoa na Wilaya waendelee kuwepo lakini wachaguliwe na wananchi na waengine wakasema wawepo na waendelee kuteuliwa na Rais kama ilivyo sasa. Tume ilitafakari kuhusu suala hili na kuamua kwamba siyo suala la Muungano na kwa kuwa Muundo wa Muungano imependekezwa uwe wa Serikali Tatu, Tume iliona suala la uwepo au kutokuwepo na namna ya upatikanaji wa Wakuu wa Mikoa na Wilaya lishughulikiwe na Washirika wa Muungano.

Serikali za Mitaa

Kuhusu Serikali za Mitaa, Tume ilipokea maoni kutoka kwa wananchi kuhusu kuziimarisha Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuzipatia uhuru kamili wa kujiamulia mambo yao bila kuingiliwa na Serikali Kuu. Tume ilitafakari suala hili na kuamua kwamba siyo jambo la Muungano na hivyo, litashughulikiwa kwenye Katiba za Washirika wa Muungano.

Uraia wa Nchi mbili

Ndugu Wananchi,
Jambo la tatu ni Uraia wa Nchi mbili. Tume ilipokea maoni kutoka kwa wananchi mbalimbali kuhusu kuwekwa kwenye Katiba suala la Uraia wa nchi mbili. Baada ya kufanya uchambuzi kwa kutengenisha mambo yapi ni ya Kikatiba na yapi yanaweza kutekelezwa bila kuingizwa kwenye Katiba bali kwenye Sheria inayohusu jambo husika, Tume imependekeza kuwa suala la Uraia wa nchi mbili linaweza kuwekwa kwenye Sheria badala ya kuwekwa kwenye Katiba. hii ni kwa sababu kutokana na utafiti uliofanywa na Tume, suala hilo linaweza kubadilika wakati wowote na hivyo likiwa kwenye Katiba linaweza kuifanya Katiba kubadilishwa mara kwa mara.

MWISHO

Naomba nichukue fursa hii kwa niaba ya Tume kuwashukuru Watanzania wote kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Mabadiliko ya Katiba, kuanzia hatua ya kutoa maoni na kuwachagua wawakilishi wenu watakaopata fursa ya kuipitia, kuijadili na kuitolea maoni Rasimu ya Katiba. Ushirikiano huu ulikuwa muhimu sana kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba hasa ukizingatia kuwa lengo ni kupata Katiba Mpya ambayo itaakisi ndoto na matakwa ya Wananchi wa Tanzania.

Tume ya Mabadiliko ya Katiba, inatoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar:

Kwa kuipatia vifaa afisi na mahitaji ya lazima
Kwa kuiwezesha Tume kutekeleza majukumu yake kwa ukamilifu,
Kwa kutokuingilia Uhuru wa Tume wakati wa Utekelezaji wa Majukumu yake na
Kutoa Wataalam wenye Weledi, Mahiri, Makini na Waadilifu ambao wameunda Sekretarieti ya Tume.

Ndugu Wananchi,
Shukrani za pekee ziwaendee:

Wakuu wa Mikoa,
Wakuu wa Wilaya,
Wakurugenzi / Makatibu wa Mamlaka za Serikali za Mitaa,
Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Wilaya,
Watendaji wa Kata, Vijiji, Mitaa na Masheha.

Kwa kuisaidia Tume kutekeleza Majukumu yake kwa ufanisi. Aidha, tunazishukuru Asasi za Kiraia, Taasisi, Jumuiya za Kidini, Vyama vya Siasa na Makundi mbalimbali kwa namna walivyoshiriki katika kuhamasisha wananchi kushiriki katika kutoa maoni.

Mwisho ingawa siyo kwa umuhimu, Tunawashukuru Wanahabari wote kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kuisaidia Tume kufikisha taarifa mbalimbali za Tume kwa Wananchi na katika kuhamasisha Wananchi kushiriki katika mchakato wa Mabadiliko ya Katiba.

Nachukua nafasi hii kuwaomba Wananchi kupitia Mabaraza ya Katiba ya Wilaya, Mabaraza ya Katiba ya Asasi, Taasisi na Makundi ya Watu wenye Malengo yanyofanana kushiriki vyema, kwa umakini, utulivu na kwa amani katika hatua hii ya kuipitia, kuijadili na kuitolea maoni Rasimu ya Katiba.

Tume imekuwa ikithamini na itandelea kuthamini mawazo na maoni kutoka kwa Watanzania wote.

Rasimu ya Katiba itapatikana kwenye tovuti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya
http://www.katiba.go.tz

SASA NAKUOMBA MHESHIMIWA MAKAMU WA RAIS UIZINDUE RASMI RASIMU YA KATIBA

Ahsanteni kwa kunisikiliza.

TOA MAONI TUPATE KATIBA MPYA

Saturday, June 1, 2013

Kigogo CUF mbaroni kwa vurugu za Mtwara

Jeshi la Polisi nchini linadaiwa kumkamata Mwenyekiti wa Jumuiya ya Vijana wa Chama cha CUF, Katani Ahmed Katani jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za uchochezi na kumsafirisha kwa ndege kwenda mkoani Mtwara.
Habari zilizolifikia Mwananchi Jumamosi na kuthibitishwa na Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro zilieleza kuwa Katani alikamatwa juzi mchana baada ya kupigiwa simu na maofisa wa polisi wa Kituo Kikuu cha Polisi jijini humo.
 
Hata hivyo Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alipoulizwa juu ya kukamatwa kwa kiongozi huyo alisema hana taarifa huku akiomba apewe muda ili aulize.
“Sina taarifa ngoja niulize”, alisema kwa kifupi na hata alipotafutwa baadaye hakupokea simu yake ya mkononi.
“Alipigiwa simu juzi na maofisa wa polisi na kuelezwa kuwa anahitajika kituoni hapo, lakini alipofika alikamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi” zilieleza habari hizo na kuongeza;

“Alihojiwa kwa saa kadhaa na jana asubuhi alisafirishwa kwa ndege kupelekwa mkoani Mtwara. Walitaka kumsafirisha kwa basi lakini viongozi wa CUF walikataa jambo hilo, hivyo kulazimika kusafirishwa kwa ndege.”

Habari hizo zilifafanua kwamba kwamba sababu kubwa ya kukamatwa kwa Katani ni kuhusishwa na vurugu zilizotokea mkoani Mtwara kati ya wananchi wanaopinga mradi wa bomba la gesi kutoka mkoani humo kwenda Dar es Salaam dhidi ya polisi.

Kwa upande wake Mtatiro alisema kuwa CUF hivi sasa inajipanga kuweka mawakili kabambe kwa ajili ya kumtetea kiongozi huyo wa vijana wa chama hicho.

“Tulijua tu kuna kiongozi wa chama atakamatwa maana kwa muda mrefu Polisi wamekuwa wakisema kuwa watawakamata viongozi wa juu wa chama. Kwa sasa Katani yupo Mtwara na sababu ya kukamatwa kwake ni kutuhumiwa kuchochea vurugu za Mtwara” alisema Mtatiro.

source: mwananchi


Thursday, May 30, 2013

Kinachodaiwa kumuua Msanii Mangwea hiki hapa

 
Dar es Salaam. Wakati mazishi ya mwanamuziki marehemu Albert Mangwea(28) maarufu kama `Ngwair’ yakitarajiwa kufanyika mjini Morogoro, maeneo ya Kihonda baada ya mwili kuwasili nchini, hospitali iliyomfanyia vipimo imethibitisha kuwa pombe na dawa za kulevya kupita kiasi ndivyo vilivyomuua.
Mwili wa mwanamuziki huyo, ambaye alitamba kwenye miaka ya 2000 na wimbo wa `Mikasi’, unatazamiwa kuletwa kesho nchini na kuagwa Jumamosi kabla ya kusafirishwa kwenda kwao Kihonda, Morogoro kwa mazishi.
Kwa mujibu wa taarifa Mangwea alifariki dunia juzi kwenye Hospitali ya St Hellen, iliyopo Johannesburg, Afrika Kusini alikokuwa amekwenda kwa shughuli za muziki.
 
Kifo chake
Ripoti iliyochapwa na mitandao mbalimbali ya ndani na nje ya nchi inasema marehemu alifikwa na umauti baada ya kulewa kupindukia, kibaya zaidi alikuwa hajala.
Siku ya kifo chake, Mangwea alianguka nyumbani kwa rafiki zake akiwa katika hali hiyo ya kulewa sana.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, baada ya kufikishwa hospitalini, Mangwea aligundulika kulewa mara tano ya kipimo cha kilevi kilichopitishwa na serikali ya Afrika ya Kusini, ambacho ni 416mg za pombe kwenye kila milimita 100(kwa mlevi anayeendesha chombo cha moto).
Pia marehemu alikutwa na upungufu wa hewa ya oksijeni kwenye seli na tishu za mwili wake.

Ripoti hiyo ilibainisha kuwa Mangwea, maarufu Ngwair, alikuwa na tatizo la kutokula chakula vizuri kabla ya kifo chake na pia kukosa muda wa kupumzika.

Sampuli zilizopatikana mwilini mwake zinaonyesha mkusanyiko wa dawa za kulevya mbalimbali zikiwemo heroine, cocaine chafu na bangi ya gramu 0.08 ambavyo vilikutwa kwenye damu yake.

Kifo chake kilitokana na mshtuko wa moyo na kushindwa kupumua, hali iliyosababisha mapigo ya moyo wake kusimama kwa sekunde chache, na kusababisha kifo chake.

Mwili wa Ngwair ulionekana kana kwamba alitokwa na damu nyingi puani baada ya kuonyeshwa kwa Watanzania wengi jana jioni Johannesburg, Afrika Kusini.

Taarifa za awali zilizotolewa na rafiki wa karibu aliyepo nchini Afrika Kusini, aliyejitambulisha kwa
 jina moja tu la Jonathan zilidai kuwa marehemu hakuamka tangu alipopumzika usiku wa kuamkia juzi.

Endelea: Mwananchi

Friday, May 24, 2013

Wamemdharau Nyerere na Kuivunja Misingi - Sasa hawana pa Kushikilia!



 
Kwao Nyerere siyo "Baba wa Taifa" tena; kwao ni "Mzee Nyerere"; kwa watawala wetu hawa walioshindwa wanasema wamefanya mambo mengi sana ya maendeleo kuliko "Wakati wa Nyerere". Wanajitamba kuwa wao wamekuza sana demokrasia na kuwa hata "Nyerere" hakuweza kufanya waliofanya wao. Katika upotofu wao wanaamini kabisa kuwa wao wanapendwa zaidi; na wanapendwa kwa sababu wamefanya mengi mno na hawaelewi kwanini watu hawaoneshi shukrani!

 Ndio maana kila kukicha hawaachi kubembeleza kwa wananchi kuwa "hamuoni tunayofanya" na kuwa watu wanalaumu tu lakini hawatoi pongezi kwa "mazuri mengi". Imefika mahali Kikwete mwenyewe amedai mahali fulani anataka kukumbukwa kuwa ni "bwana maendeleo"; anasema hivi kwa sababu anapokaa ofisini anaamini kabisa kuwa ameweza kuwapatia Watanzania 'vitu" vingi sana vya maendeleo kuliko wakati wowote wa historia - vitu ambavyo hata Nyerere hakuweza kuwapatia. Kikwete anataka awe juu ya Nyerere kwa kila kipimo kwani kipimo kilichowekwa ni Nyerere. Na bila ya shaka kuna sababu - Nyerere hakuamini kuwa walikuwa tayari kuwaongoza Watanzania - hawa kina Kikwete na Lowassa.

 Sasa katika kumdunisha Nyerere ili wao wakue wameacha propaganda chafu dhidi ya Nyerere na uongozi wake. Leo hii tunashuhudia mambo ambayo - pamoja na 'ubaya' wote wa Nyerere hayakuwahi kutokea chini ya "dhaalim Nyerere"! Matukio yanayotokea leo hii ukiwaambia watu walioshi wakati wa Nyerere, chini ya chama kimoja na uongozi thabiti hawawezi kuelewa yanawezekana vipi kutokea. Watu wa enzi za Mwalimu wanakumbuka vizuri kuwa kiongozi aliyefanya madudu hakuvumuliwa; na bahati mbaya wakati ule hatukuwa na wasomi wengi na watu wengi wenye udhoefu lakini Nyerere hakuwaonea huruma. Wapo ambao hadi leo wana kinyongo na Nyerere kwa sababu hakuwapa nafasi nyingine.

 Lakini katika kumdharaulisha Nyerere na kujaribu kupuuza mafanikio yake makubwa zaidi wamejikuta hawana pa kukimbilia! Tuliokuwa wakati wa Nyerere hatukumbuki jinsi JWTZ likitumiwa kisiasa kama linavyotumika hivi sasa! Fikiria ndege ya jeshi itumwe kumchukua raia kumpeleka Mahakamani!? Kwamba, ati vurugu za uchaguzi zilazimishe JWTZ kuingilia kati! Kwamba vikosi vya kutuliza ghasia vya polisi vizidiwe nguvu na mara moja kuliingiza jeshi kufanya kazi za jeshi la polisi! Unthinkable! Lakini wao wanaamini wako sawa!

 Lakini siyo kwamba wamedharaulisha na kumtupa nje Nyerere ni zaidi ya hivyo; wameitupa misingi ya taifa letu. Wanataka kujenga kwa misingi ya mabua! Waliachiwa misingi ya zege lakini wao wakiamini ni 'magenius" wameamua kutengeneza 'taifa jipya' nje ya misingi iliyounda Tanzania. Leo hii Watanzania kwa mamilioni wananung'unika moyoni kwani hawatambui kama hili ndilo Taifa waliloachiwa kama urithi. Sasa hivi inaonekana Tanzania inazidi kufanana zaidi na mataifa mengine ya Afrika kiasi kwamba linaweza lisitofautike tena mbele ya umma.

 Wameitupa misingi sasa hawana cha kujengea; wamebakia kutumainia vitisho, dharau na matumizi ya nguvu. Wameshindwa kabisa kujenga hoja - kwa mfano kwenye hili suala la gesi. Hawana ushawishi wa hoja na badala yake hata kauli zao wanazotoa zimejaa dharau (contempt) na matokeo yake watu nao wanawadharau! Wanafikiri vitisho na kejeli zinajibu hoja!

 Kushindwa kwa sera zao mbalimbali ni matokeo ya kuachana na misingi ya taifa; wanafikiri wanaweza kutengeneza sera nzuri nje ya misingi ya taifa! Matokeo yake:

 Sera ya Nishati na Madini imeshindwa

 Sera yao ya Gesi imeshindwa - hata kabla haijaanza!

 Sera yao ya Elimu imeshindwa
 Sera yao ya siasa imeshindwa
 Sera yao ya Sayansi na Teknolojia imeshindwa
 Sera yao Mazingira imeshindwa
 N.k

 Wameshindwa lakini hawaamini wameshindwa na badala yake wanawalaumu wanaowaambia wameshindwa kwa kushindwa kwao! Kana kwamba, wanaowalaumu wakinyamaza basi wao wataweza! Wenyewe wanaambizana kuwa wakipewa nafasi nyingine 2015 basi wataaanza kuweza; na wapo watu wanaamini kuwa hilo linawezekana; kwamba pundamilia anaweza kugeuka na kuwa farasi! Kama wenyewe wameshindwa kuvuana magembe licha ya mbwembwe zote za "kuvuana magamba" kweli kuna uwezekanow wataweza? Na ukweli ni kuwa walipofika sasa hawawezi kurudi kwenye misingi ya Nyerere na Taifa letu; kwa sababu kurudia misingi hiyo ni kujishtaki katika historia.

 kuna namna moja tu ya kuwasaidia... kuendelea kuwakataa.

 Maskini CCM! 
 Maskini Kikwete
 Maskini Tanzania chini yao!
Source: Mwanakijiji

Wednesday, May 22, 2013

Bajeti nishati

 
Dodoma/Mtwara.
Wakati mjadala mkali ukitarajiwa kuibuka bungeni leo wakati Serikali itakapokuwa ikiwasilisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, joto limezidi kupanda mkoani Mtwara ikielezwa kuwa wananchi wamehamasishana kwa mara nyingine kuacha shughuli zote ili kusikiliza kama hotuba hiyo italinda masilahi yao.
Hotuba hiyo ambayo itasomwa leo mara baada ya kipindi cha maswali na majibu bungeni na Waziri wa wizara hiyo, Profesa Sospeter Muhongo, inatarajiwa kuibua mengi yakiwamo yanayohusu suala la gesi ya Mtwara.
 
Mjini Mtwara vipeperushi vinavyopingana vilisambazwa kuhamasishana ‘kuacha shughuli zao zote na kubaki nyumbani ili kufuatilia matangazo ya televisheni wakati Profesa Muhongo atakapotangaza bajeti hiyo, huku vingine vikipinga.
 
Ahadi za matumaini
Licha ya kampeni hizo za watu wa Mtwara, Serikali nayo imeweka matangazo katika vyombo vya habari likiwemo gazeti hili ikieleza namna mikoa ya Mtwara na Lindi itakavyonufaika na utafutaji na uendelezaji wa Gesi Asilia.
Tangazo lililotolewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania limeainisha faida za gesi hiyo kwa Mkoa wa Mtwara ukiwamo umeme utakaotokana na gesi asilia. Pia imeelezwa jinsi mafunzo kwa vijana juu ya matatizo ya gesi asilia yaliyodhaminiwa na Wizara ya Nishati na Madini na kampuni mbalimbali kuanzia mwaka 2010.
Vilevile imeelezwa jinsi uboreshaji wa huduma za jamii kama ujenzi wa shule, hospitali na ujenzi wa viwanda kama kile cha saruji cha Dangote na mitambo ya kusafishia gesi utakavyowanufaisha wakazi wa mkoa huo.

Gesi hiyo ambayo pia inachimbwa katika Kisiwa cha Songosongo inatajwa kwamba itawanufaisha wakazi wa Mkoa wa Lindi kwa kupata umeme, kunufaika na kodi ya wawekezaji wa gesi na udhamini wa mafunzo kutoka kampuni mbalimbali na wizara.
Wiki iliyopita Profesa Muhongo alijigamba kuwa bajeti ya wizara yake atakayosoma leo itakuwa ya karne ya 22 itakayomaliza tatizo la umeme nchini kwa kuwa imetoa vipaumbele kwa sekta binafsi kusaidia upatikanaji wa umeme wa uhakika.

Wabunge wapania
Dalili za kuibuka mjadala mkali katika bajeti ya leo zilianza kujitokeza mwishoni mwa wiki wakati wa semina ya wabunge kuhusu masuala ya gesi ambapo wizara hiyo ilibanwa juu ya mambo ya mikataba.
Hata hivyo, semina hiyo ilitafsiriwa kuwa ililenga kuwapoza wabunge na kupunguza hasira zao huku wizara ikijipanga namna ya kuwashawishi waikubali bajeti baada ya kuona mwelekeo wao.

Wasiwasi Mtwara
Hali ya wasiwasi imeanza tena kutanda mkoani hapa hasa kutokana na vipeperushi vinavyokinzana na ujumbe tofauti kwa njia ya simu unaosambazwa.
Hali hiyo imejirudia tena huku ikionekana dhahiri kuwa na kauli kutoka makundi tofauti zinapishana katika vipeperushi hivyo huku wengine wakitaka mwendelezo wa kusitisha huduma ufanyike na wengine wakipinga.
Mojawapo ya kipeperushi kilisisitiza huduma zote zisitishwe kuanzia bajaji, bodaboda, masoko na magari yote yaendayo mikoani na wilayani yasiingie wala kutoka.
 
Huku vipeperushi vingine vikipinga: “Tunafahamu gesi ni mali yetu wote Wanakusini na tunafahamu kunyanyasika kwetu na Serikali ya nchi yetu na Mei 17 tuliunga mkono kufunga maduka na biashara zote, lakini hatukunufaika na chochote.
“Sasa Jumatano tena tusifanye biashara. Tuache ujinga Wanakusini wenzetu wengine hawana kazi wala gesi. Kampeni zitafanya tuwe maskini zaidi. Tarehe 22.05.2013 hatufungui duka wala hoteli, hata soko,” kilisomeka kimoja kati ya vipeperushi hivyo.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Linus Sinzumwa aliwataka wananchi waendelee na shughuli zao za kila siku bila kujali vitisho hivyo kwa kile alichokidai kuwa ulinzi umeimarishwa.

mwananchi

Wednesday, May 15, 2013

Kumwongezea JK muda

 
Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahimu Lipumba amedai kuwa amenasa taarifa za siri za kuwapo kwa mipango ya kuongeza muda wa Serikali ya sasa kukaa madarakani.
Profesa Lipumba alisema hiyo inatokana na wasiwasi kuwa mchakato wa Katiba Mpya hautaweza kukamilika mwaka 2014 hivyo kutokuwa rahisi kwa uchaguzi kufanyika mwaka 2015.
Akizungumza Dar es Salaam jana, wakati akifungua kikao cha Baraza Kuu la CUF, Profesa Lipumba alisema kuwa Serikali inataka kuongezewa muda wa kukaa madarakani kwa miaka miwili ikimaanisha kuwa Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kikwete itakaa madarakani hadi mwaka 2017.
 
Hata hivyo, madai hayo ya Profesa Lipumba yamepingwa vikali na Serikali na viongozi wake watatu waandamizi ambapo walijibu walipoulizwa kwa maandishi na mwandishi wetu mjini Dodoma wanakohudhuria kikao cha Bunge.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe alijibu: “Mchakato wa Katiba upo ‘on track’ (unakwenda vizuri) hatuna sababu ya kufanya hivyo.”
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alijibu” “Njooni ofisini kwangu nitasema ni kitu gani.”

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi alijibu kwa utani bila ya kufafanua: “Njooni niwajuze, unajua kamba haitoki Ukambani kama ilivyo kamba.”

Profesa Lipumba amemwomba Rais Kikwete asilikubali wazo hilo akisema wananchi hawatakubali na taifa linaweza kuingia katika mtafaruku.

“Nitapenda kuona Rais Kikwete akikataa jambo hilo kwani litachafua taswira ya nchi. Hatua hii ni kinyume cha utawala bora,” alisema Profesa Lipumba.

Alisema Serikali haipaswi kuhofia uchaguzi kwa sababu ya Katiba kwani bado uwezekano wa kuandaa uchaguzi wa haki na huru unawezekana kwa utaratibu mwingine.

“Mchakato wa Katiba unaendelea, Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatuambia kwamba mwaka 2014 tutakuwa na Katiba Mpya, sasa CUF tunasema kwamba hata kama Katiba Mpya haitapatikana kwa kipindi hicho kuwe na Tume huru ya Uchaguzi,” alisema Profesa Lipumba.

source:mwananchi

Friday, May 10, 2013

‘Mkutano wa amani ni ‘porojo’: Mtikila

 
Dar es Salaam. Wakati Mkutano wa Viongozi mbalimbali wa dini na Jeshi la Polisi ukimalizika jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Chama cha Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila amesema mkutano huo ulioitishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Said Meck Sadick, umejaa porojo na kwamba hauwezi kuleta suluhu yoyote.
Kwa siku mbili, viongozi hao wa kidini walikuwa wakijadili masuala ya amani ya nchi baada ya kutokea tofauti mbalimbali pamoja na kuwapo mazingira ya kuhatarisha amani nchini.
Akizungumza Dar es Salaam jana akiwa nje ya ukumbi wa mkutano huo, alisema kwa kawaida imani ya mtu ipo ndani ya roho yake na huwezi kuiondoa kwa maneno au kufanya mikutano bali kinachotakiwa ni Serikali kujitahidi kuondoa makosa yaliyojitokeza siku za nyuma ambayo ndiyo yamezaa tofauti zinazojitokeza.
                              
“Mimi nadhani mkuu wa mkoa na chama chake kukaa na kufikiria kuitisha mkutano wa viongozi wa dini wenye lengo la kumaliza tofauti za dini ambazo zinajitokeza haupo sahihi kwani ni vyema tatizo likaangaliwa lipo wapi ili kupata majibu sahihi ya tofauti zinazojitokeza sasa,” alisema Mtikila. Mkutano huo ulitarajiwa kufungwa jana na Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi.

Alisema katika mkutano huo hakutakuwa na suala jipya kwani kila kitu kipo wazi na kwamba tatizo linalojitokeza wakati huu ni la muda mrefu tangu mwaka 1986 ambapo aliwahi kusema masuala ambayo yatakuja kujitokeza siku za usoni ikiwamo suala la udini.

“Mimi nadhani kwamba kuna haja ya msingi kuangalia suala hili la imani za kidini kwa undani hasa kutafuta tatizo lipo wapi,lakini siyo mtu mmoja akae na na kufanya mkutano kwa lengo la kutafuta suluhu ya migogoro ya dini wakati si jambo rahuisi kiasi hicho,”alisema.

Source: Mwananchi
 
 

Wednesday, May 8, 2013

Bomu Arusha: Pengo afichua siri


Dar es Salaam/Arusha. Kadinali Pengo alisema amepata taarifa kutoka kwa watu ambao hana na shaka nao.

“Jana (juzi), niliongelea kwamba suala zima la tukio la Arusha halihusiani na imani yoyote ya kidini. Tamko hilo nilitamka kutokana na taarifa nilizofikishiwa na watu ambao sikuweza kuwa na shaka kwamba wanaoniambia ni kweli na sidhani kama ningekuwa na sababu ya kusema wamefika kwa kunidanganya kwa hiyo tamko litakuwa limesimama juu ya msimamo huo,” alisema Kadinali Pengo na kuongeza:

“Lengo la msingi kabisa, langu na la kanisa ni kwamba tukio lolote lile liwe kwa nia mbaya au nzuri kwa upande wetu isiwe ni sababu ya kuanza mapambano na kuwa chimbuko la ukosefu wa amani katika nchi yetu,” alisema Pengo.
 
Alisema kuwa kila anayehusika ajue amani ya kweli ya taifa lolote haiwezi ikapatikana isipokuwa ikijengwa juu ya ukweli na ukweli kabisa bila kufuta au kujaribu kupotosha ukweli kwa namna yoyote ile.

“Tusipojua kusema ukweli ulivyo hatuwezi kufaulu kuleta amani katika taifa letu. Kwa hiyo pamoja na kuendelea kuwaomba waumini wa Katoliki pamoja na watu wenye mapenzi mema kuendelea kumwomba Mwenyezi Mungu arehemu taifa letu na mapambano ya aina yoyote ile. Tuendeleze nia yetu njema ya kusema ukweli, haidhuru ukweli huu unamgusa nani,” alisema Pengo.
 
Alisema kujaribu kuficha ukweli na kupotosha ni njia sahihi kwa ibilisi kuleta vurugu katika jumuiya ya watu na ieleweke hivyo.

“Naomba kila mtu akubaliane na tamko langu haidhuru pana kosa, amani ya taifa letu ni jambo la msingi na amani itajengwa tu iwapo kila mtu anayehusika atakuwa tayari kusema ukweli kama ulivyo,” alisema.

Mwingine afariki, 20 wakutwa na vipande vya chuma miilini
Katika hatua nyingine, majeruhi mmoja katika shambulio hilo lililotokea Jumapili iliyopita, amefariki dunia juzi jioni na kufikisha idadi ya waliopoteza maisha kufikia watatu.

Aliyefariki ni mtoto wa miaka tisa, Patricia Joachim ambaye alikuwa amehamishiwa Hospitali ya Rufaa ya KCMC, Moshi. Wengine waliofariki katika tukio hilo ni Regina Losyoki (45) na James Gabriel (16).

Mazishi ya watu hao watatu yamepangwa kufanyika katika eneo la kanisa hilo Ijumaa.
Katika hatua nyingine, majeruhi 20 wamebainika kuwa na chembechembe za vyuma walivyopata katika shambulio hilo. Hao ni miongoni mwa majeruhi 42 waliolazwa hadi sasa kwenye hospitali mbalimbali za Arusha.
 
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mount Meru, Dk Thomas Kway alisema majeruhi hao 20 wamedhuriwa na chembechembe za vyuma vya mabomu na baada ya miili yao kubainika kuwa na vyuma vyenye urefu hadi wa sentimita tisa.

Dk Kway alisema hayo wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipofika katika hospitali hiyo kuwafariji majeruhi hao.

Kutokana na hali hiyo, Pinda aliwataka madaktari waliowafanyia upasuaji majeruhi waliolipuliwa na bomu kuhifadhi vipande hivyo ili vitumike katika uchunguzi.

Aliwaambia wabunge kuwa vyuma hivyo vitasaidia upelelezi ili kufahamu aina ya bomu lililotumika.
“Tumeamua kuwa vipande vya vyuma vinavyotolewa baada ya upasuaji visitupwe, vitumike kwa uchunguzi,” alisema Pinda na kuongeza kuwa baadhi ya majeruhi wamepelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.
 
Waliokamatwa
Akitoa taarifa kwa Rais Jakaya Kikwete ambaye alifika Arusha jana, Mkuu wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo alisema watu tisa wamekamatwa hadi sasa.

Aliwataja baadhi yao kuwa ni Victor Ambrose na wengine aliowataja kwa jina mojamoja ni Joseph na David.

Alisema wengine ni raia watatu wa Saudi Arabia, ambao walikuwa na wenyeji wao wawili na Watanzania wengine watatu.

Kauli ya Kikwete
Akizungumza Arusha jana, Rais Kikwete amewataka waumini wa dini zote waendelee kusali akiahidi kwamba Serikali itaimarisha ulinzi. Alisema amekerwa na kukasirishwa na tukio hilo.

Rais Kikwete alitanguliwa kufika Arusha na Makamu Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Shariff Hamad na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd ambao pia walitembelea Kanisa lililolipuliwa na baadaye kwenda kuwatembelea wafiwa na kuwafariji majeruhi hospitali.

Viongozi wote hao walitoa wito kwa Watanzania kulinda amani iliyopo na kuacha malumbano ambayo hayana tija kwa maslahi ya taifa.
Chanzo: Mwananchi

Tuesday, May 7, 2013

CCM ndio chanzo cha Udini: Zitto


Mbunge wa Kigoma kaskazini na naibu katibu mkuu wa CHADEMA mh Zitto Kabwe jana alikituhumu wazi wazi Chama Cha Mapinduzi kuwa ndio kiini cha udini unaoanza kuligubika taifa la Tanzania lililokuwa linasifika kwa amani.
 
Akichangia hoja ya makadirio ya bajeti ya wizara ya mambo ya Ndani jana usiku Bungeni mjini Dodoma, Zitto alisema CCM imekuwa na tabia ya kuvihusisha vyama vya upinzani vyenye nguvu na udini. "Wakati chama cha wananchi CUF kilipokuwa na nguvu kilihusishwa na dini ya kiislamu, vivyo hivyo kwa CDM ambacho kinahusishwa na dini ya kikristo pamoja na ukanda" alisema Mh Zitto.
 
"Hali hii bila kujua ndi imeleta mifarakano ya kidini miongoni mwa jamii yetu hivyo kupelekea kuwa na chuki kubwa miongoni mwa dini hizi mbili na kusababisha matukio ya ajabu kutokea katika nchi yetu" Alisema Mh Zitto.
 
Hata hivyo Zitto kwa kiasi kikubwa aliwalaumu viongozi wote kwa ujumla kuacha kutoa hotuba zenye kuchochea chuki miongoni mwa jamii ya Tanzania na kubadilika mara moja ili kuijenga upya jamhuri ya muungano wa Tanzania ambayo kwa sasa ina nyufa nyingi zinazoweza kuliangusha taifa hilo nguli la Amani.

Wasaudia wanne mbaroni, FBI watua Arusha


Dodoma/Arusha. Wakati maofisa wa Shirika la Upelelezi wa Marekani (FBI) wametua Arusha, raia wanne wa Saudi Arabia na Watanzania wawili wamekamatwa kwa tuhuma za kuhusika kulipua bomu lililoua watu wawili na kujeruhi wengine 61 wakati wa ufunguzi wa Kanisa la Mtakatifu Joseph Parokia ya Olasiti.

Waliofariki dunia ni Regina Longino Kurusei (45), mkazi wa Olasiti na James Gabriel (16), ambaye alifariki usiku wa kuamkia jana.

Tukio hilo lilitokea wakati Balozi wa Vatican na Mwakilishi wa Papa nchini, Francisco Montecillo Padilla alipokuwa akizindua kanisa hilo.

Akitoa maelezo kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda jana, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo alisema raia hao wa Saudi Arabia walikamatwa jana asubuhi baada ya tukio wakiwa kwenye gari wakielekea Kenya kupitia Namanga.

Mulongo alisema raia hao wa kigeni waliingia nchini Jumamosi iliyopita na siku iliyofuata ndipo kukatokea ulipuaji huo. Alisema lengo la shambulizi hilo lilikuwa kumdhuru Askofu Padilla.
 
“Mtu ambaye tulimkamata jana (juzi Jumapili) ndiye aliyesaidia kuwapata watu hawa wa Saudi Arabia na Watanzania hao,” alisema Mulongo.

Mulongo alisema maofisa wa FBI walifika jana saa tano asubuhi ili kusaidiana na Polisi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), katika uchunguzi wa tukio hilo.
Maofisa hao wa FBI walikuwa Zanzibar ambako walikuwa wanachunguza kifo cha Padri Evaristus Mushi ambaye aliuawa Februari 17, mwaka huu.

Hii itakuwa mara ya pili kwa wageni kuhusishwa na matukio ya ugaidi nchini baada ya mwaka 1998 wakati raia kadhaa wa Misri wakiongozwa Fazul Abdulla waliposhirikiana na Watanzania kadhaa akiwamo Ahmed Ghailani kulipua ubalozi wa Marekani nchini na ule wa Kenya. Ghailani anatumikia kifungo cha maisha nchini Marekani wakati Fazul aliuawa Somalia mwaka 2011.

Tamko la Serikali
Akitoa tamko la Serikali bungeni jana, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi alimtaja mmoja wa watuhumiwa wanaoshikiliwa kuhusika na tukio hilo kuwa ni Victor Calisti Ambrose (20), mkazi wa Kwa Mrombo Arusha ambaye ni dereva wa bodaboda. Alisema kijana huyo ndiye anayetuhumiwa kurusha bomu hilo.

Waziri Nchimbi alitoa onyo kali kwa wanasiasa wanaopandikiza chuki za kidini miongoni mwa Watanzania na kuishutumu Serikali kutokana na matukio kama hayo. “Kuna wanasiasa ambao wanaona masilahi yao ni muhimu kuliko maisha ya Watanzania, masilahi yao ni muhimu kuliko utulivu wa Watanzania na masilahi yao ni muhimu kuliko umoja wa Watanzania.”
 
JK akatiza ziara, Bilal atoa ahadi
Rais Jakaya Kikwete, amekatiza ziara yake ya kiserikali nchini Kuwait ili kurejea nyumbani kutokana na shambulio la bomu kwenye kanisa hilo.

Taarifa ya Ikulu imesema jana kwamba Rais Kikwete amelazimika kukatiza ziara hiyo na kurejea nyumbani mara moja ili kuwa karibu na wafiwa pamoja na wale waliojeruhiwa katika shambulio hilo la kigaidi.

Makamu wa Rais, Dk Gharib Bilal ameahidi kuwa Serikali itahakikisha wote waliohusika na tukio hilo wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya dola.

Balozi wa Papa atoa tamko
Askofu Padilla ambaye jana alitembelea majeruhi katika Hospitali ya Mkoa, Mount Meru, alieleza kustushwa na tukio hilo na kusema hakutarajia kitu kama hicho kutokea wakati wa shughuli hiyo wakati Watanzania wakijulikana ni watu wa amani.
Alilaani tukio hilo na kuvitaka vyombo vya usalama kufanya uchunguzi ili kubaini ukweli.

Kanisa Katoliki Arusha
Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha jana liliitaka Serikali iwataje waliohusika na tukio hilo la kigaidi huku likiwataka waumini wake kutolipiza kisasi.

“Msimamo wa kanisa katika hili, ni kuwataka waumini wasilipize kisasi kama ambavyo alisema Yesu Kristo kuwa msilipize kisasi, muwe tayari kushinda ubaya kwa wema,” alisema Askofu Josephat Lebulu na kuongeza:
EU
Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU), imetaka kuharakishwa kwa uchunguzi wa tukio hilo na kuonya kuwa matukio kama hayo yanaweza kulitumbukiza taifa kwenye machafuko.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Balozi wa Umoja huo nchini, Filiberto Ceriani-Sebregondi alisema Tanzania inapaswa kufahamu kwamba pasipo kujenga, kuendeleza na kusisitiza utamaduni wa kuvumiliana, hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwa siku za usoni.
 
Source: Mwananchi

Tuesday, April 30, 2013

Maji moto kwa Serikali

 
Dodoma. Bajeti ya Wizara ya Maji jana ilipita kwa mbinde baada ya kukwama mara mbili bungeni.Imepita baada ya Serikali kuongeza Sh184.5 bilioni kama Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji ilivyokuwa imependekeza na kuungwa mkono na wabunge wengi.

Awali, Bajeti hiyo ilikwama kupitishwa tena katika kipindi cha jana asubuhi baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kukatiza mjadala wake kutokana na wabunge kuibana Serikali kwa kukiuka vipengele kadhaa wakati ilipowasilisha upya hoja hiyo.

Mara ya kwanza Bajeti hiyo ilikwama wiki iliyopita baada ya wabunge kushinikiza kuongezwa kwa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya kusambaza maji vijijini.

Jana asubuhi, Makinda alisitisha shughuli za Bunge saa 5.45 asubuhi ikiwa mapema kabla ya muda wa kawaida wa kumalizika kwa vipindi vya asubuhi ya Bunge ambao ni saa 7.00 mchana baada ya wabunge kupinga utaratibu wa uwasilishaji upya wa Bajeti hiyo.

Licha ya Serikali kuongeza Sh184.5 bilioni, bado baadhi ya wabunge wa Chadema waliomba Bajeti hiyo iahirishwe kujadiliwa wakisema nyongeza hiyo haina ushahidi wa utekelezaji
 
Baada ya Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa kuwasilisha kauli ya Serikali kuhusu kuongeza fedha kwenye Bajeti ya Wizara ya Maji na Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe kusoma marekebisho ya bajeti yake na kujibu hoja mbalimbali za wabunge, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe alihoji sababu za Serikali kuwasilisha kauli ya kuongeza fedha bila kuwagawia wabunge nakala kama kanuni zinavyotaka.

“Mwaka juzi tulitaka fedha ziongezwe Wizara ya Uchukuzi na Serikali ikasema imeongeza Sh94 bilioni na tukapiga makofi sana hapa, lakini haikuongezwa hata senti moja.”

Pia, Zitto alisema mwaka 2011 walikubaliana fedha zinazotokana na ushuru wa mafuta ya taa kupelekwa Wakala wa Umeme Vijijini (Rea), lakini hakuna kilichopelekwa mpaka sasa.

Kutokana hali hiyo, alitaka hoja hiyo kutolewa kwa maandishi na wabunge wapewe nakala zake ili waibane Serikali pale itakaposhindwa kutekeleza.

Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu ambaye alitinga bungeni baada ya kutumikia adhabu ya kusimamishwa kwa siku tano, alisema kwa mujibu wa taratibu za Bunge, kauli za Serikali lazima zisambazwe kwa wabunge tofauti na kauli ya Waziri wa Fedha akisema hata Spika hakuwa na nakala yoyote huku akisema Waziri alitoa kauli hiyo akiwa hana anachokisoma.

Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika alitaka hoja hiyo kuondolewa mezani kwa sababu Waziri wa Maji wakati akifanya majumuisho ya hoja yake, hakutoa jedwali linaloonyesha matumizi ya fedha hizo.
 
Akitoa mwongozo wake, Spika Makinda alisema Waziri wa Fedha alitoa tamko la Serikali bila wabunge kuwa na nakala kutokana na haraka iliyokuwapo... “Tuliona haiwezekani Waziri wa Maji aseme peke yake juu ya ongezeko la fedha hizo, ndiyo maana Waziri wa Fedha akaja kutoa tamko hapa.”
 
Hata hivyo, Makinda alikubaliana na hoja ya Mnyika na kuahirisha Bunge huku akitaka jedwali linaloonyesha matumizi ya fedha hizo liandaliwe.

Hata katika kipindi cha jioni, Mnyika aliendelea na msimamo wake kwa kutoa hoja akitaka kupata hakikisho la Serikali kwamba fedha hizo zitakuwapo kweli na siyo danganya toto ili kupitisha bajeti hiyo hoja ambayo iliungwa mkono na kumlazimu Waziri wa Fedha kusimama na kutoa hakikisho hilo akisema: “ Serikali itahakikisha fedha zinazopitishwa zinapatikana.”
Akiahirisha Bunge, Spika Makinda alisema fedha hizo zitatoka ndani ya Bajeti hiyo inayoendelea kujadiliwa na hazitatoka nje.

Hatua hiyo ilifanya bajeti hiyo kuondolewa kwa mara ya pili bungeni na hivyo kuingizwa kwenye kumbukumbu za bajeti zilizowahi kuondolewa kwa sababu ya kutokidhi matakwa ya hoja za wabunge.
 
Awali, Dk Mgimwa akitoa tamko la Serikali alisema wameamua kufanya maji kuwa kipaumbele kutokana na umuhimu wake.

Alisema Serikali imetafuta fedha za ziada ambazo zimetoka kwenye matumizi mengine, hasa posho ambazo hazitaathiri uendeshaji wa Serikali.

Kwa upande wake, Profesa Maghembe alisema Serikali imeongeza Sh184.5 bilioni kama ilivyopendekezwa na Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji.
 
Chanzo: Mwananchi

Monday, April 8, 2013

Harusi ya Mangula yafana......


Makamu mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Tanzania bara Philip Mangula (72), hatimaye amefunga ndoa na mkuu wa shule ya sekondari ya Philip Mangula iliyopo kata ya Imalinyi wilayani Wanging’ombe mkoani hapa, Yolanda Kabelege (54).
 
Ndoa ya Mzee Mangula na Mwalimu Yolanda imefungwa jana majira saa 8 mchana katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheli Tanzania (KKKT) mjini Njombe, ambapo misa ya ibada ya ndoa hiyo iliongozwa na Askofu Mstaafu wa KKKT dayosisi ya kusini Njombe Solomon Swalo pamoja na Askofu Isaya Mengele wa diyosisi hiyo.
 
 
 

Saturday, March 30, 2013

Balaa tena! Watu 40 wahofiwa kufukiwa baada ya jengo la ghorofa 15 kuporomoka Dar

Dar es Salaam. Watu zaidi ya 40 wanahofiwa kufukiwa na kifusi baada ya jengo la ghorofa 16 lililokuwa linajengwa kuporomoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam jana asubuhi.
 
Kuporomoka kwa ghorofa hilo lililokuwa katika Mtaa wa Indira Gandhi, kulizua huzuni, taharuki na simanzi kwa ndugu na jamaa waliofika kwenye eneo la tukio kutaka kufahamu nini kimetokea.
 
Shughuli mbalimbali katikati ya jiji hilo zilisimama kwa siku nzima baada ya jengo hilo kuanguka na kusababisha vifo vya watu watano, 13 kuokolewa huku zaidi ya watu 40 wakisadikiwa kufukiwa na kifusi cha udongo wa jengo hilo.
 
Jengo lililoporomoka
 
Jengo hilo lililokuwa likijengwa mkabala na Msikiti wa Shia Ithnasheri ulioko Barabara ya Indira Gandhi na Kampuni ya ‘Lucky Construction Limited’ lilianguka majira ya saa 2.30 asubuhi wakati ujenzi ukiendelea juu huku chini watoto wakicheza mpira na mama lishe wakiendelea na biashara zao kama kawaida.

Pamoja na vifo na wengine kujeruhiwa, magari takribani manne yalifunikwa na kifusi cha jengo hilo na kupondwa pondwa na kuwa kama chapati.
 
Katibu wa Msikiti wa huo wa Shia Ithnasheri, Mushtaq Damji alisema: “Leo tulikuwa na kitu kama jumuiya kwa jamii ya wahindu, tulipanga kusherehekea lakini yote yakafutika.
 
“Baada ya swala ya alfajiri, watu walikuwa wanazungumza hapa na pale na baada ya kupambazuka, watoto walikuwa wanacheza mpira, walikuwa 9. Sasa, bahati nzuri watoto saba wakakimbia na watoto wawili wakawa wamekwama,” alisema Damji.

Naye Mlinzi wa Msikiti huo, Athuman Nassor alisema: “Mimi nafanya kazi ya ulinzi hapa msikitini, lakini nilikuwa ninashangaa kiasi cha saruji kilichokuwa kikitumika kukorogea zege, kweli walikuwa wanazidisha mchanga.
 
“Niliwahi kuwaambia hata hawa vibarua, kuwa hii inayofanyika mbona siyo…,” alisema mlinzi huyo. Alisema; jana ilikuwa siku ya kumwaga zege ghorofa ya 16 na kulikuwa na vibarua wapatao 50 ambao kila mmoja alikuwa na ndoo yake tayari kuanza kazi kabla ya ghorofa hilo kuporomoka.
Mlinzi huyo alisema kuwa wakati tukio hilo linatokea alikuwa mbali kidogo na eneo la tukio na kusema kuwa bila shaka baadhi ya kinamama lishe ni miongoni mwa waliofukiwa.

Habari zilizopatikana baadaye jana jioni zilidai kuwa mmiliki wa jengo, Ally Raza pamoja na mhandisi wa Kampuni iliyokuwa ikijenga jengo hilo ya Lucky Construction Limited walidakwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere wakijiandaa kutimka.

Viongozi wamiminika
 
Rais Jakaya Kikwete alifika katika eneo la tukio saa 6:45 mchana na alipata maelezo mafupi ya tukio hilo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadik na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
 
Baada ya maelezo hayo, Rais Kikwete aliyetumia dakika tisa, alimwambia Mkuu wa Mkoa na Kamanda Kova: “…mmiliki na mhandisi lazima wakamatwe mara moja.”
Kikwete baadaye alitikisa kichwa kuonyesha masikitiko na kuondoka.
 
Viongozi wengine waliofika ni Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal ambaye hata hivyo hakuzungumza lolote hata baada ya kupata taarifa kutoka kwa mkuu wa mkoa.
 
Naye aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) ambaye sasa ni Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa CCM, Dk Asha-Rose Migiro alisema tukio hilo linaumiza na kusikitisha kwani limepoteza nguvu kazi ya taifa.
 
“Ni vigumu kupata maneno ambayo yatabeba uzito wa tukio hili lakini wajenzi wanatakiwa kuwa makini na ujenzi wao,” alisema Migiro.

Wananchi wajitokeza kuokoa
 
Mapema Wananchi waliojitokeza kwa kushirikiana na askari polisi na mgambo wa Jiji walioanza kuondoa kifusi cha mchanga kwa kutumia mikono kutokana na kutokuwapo kwa vifaa vya kuondolea kifusi hicho.

Endelea: Mwananchi

Thursday, March 28, 2013

Rais Tucta ang’olewa

 
Mambo siyo shwari ndani ya Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) kutokana na kutimuliwa kwa Rais wake, Ayoub Omar.

Omar alilithibitishia gazeti hili jana kuwa aliondolewa wadhifa huo kwenye kikao cha Kamati ya Utendaji cha Tucta kilichofanyika Machi 25, mwaka huu.

Alisema kuwa alivuliwa wadhifa huo baada ya kuundiwa zengwe na viongozi wenzake waliodai asingeweza kuendelea na wadhifa huo kwani hakuwa na sifa.
 
Katiba ya Tucta inaelekeza kuwa kiongozi wake lazima awe mwajiriwa katika sekta ya umma au ile ya binafsi.

Omar alisema kuwa viongozi wenzake walikuja na ajenda kuwa hakuwa na kazi kwani alikuwa amestaafu kwenye Kiwanda cha Mbolea cha Mbeya alikokuwa anafanya kazi.

“Ni kweli nilistaafu pale Kiwanda cha Mbolea lakini nilipata ajira sehemu nyingine baada ya muda mfupi,” alieleza Ayoub, ambaye kwa sasa anafanya kazi kwenye Kampuni ya Nuru Enterprise.

Ayoub alisema alisikitishwa na kitendo kile kwani anaona ni zengwe tu kwani ana sifa za kuongoza kwa kuwa ni mwajiriwa.

“Mimi naheshimu uamuzi wao ila niliwapelekea vielelezo kuwa mimi ni mwajiriwa lakini walikataa,” aliongeza Ayoub, ambaye anaendelea na wadhifa wake kama Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani (Tuico).

Katibu Mkuu wa Tuico, Nicolaus Mgaya alipoulizwa kuhusu suala hilo, alikanusha vikali kuenguliwa kwa mwenyekiti wake.

Gazeti hili, hata hivyo, linafahamu kuwa suala hilo limesababisha mgawanyiko mkubwa ndani ya Tucta.

Source: Mwananchi

Tuesday, March 26, 2013

Cheti alichotumia Mulugo cha Mhadhiri wa Mkwawa

 
Dar es Salaam. Imebainika kuwa mmoja wa watu ambao Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo (pichani)anadaiwa kutumia jina lake kutafuta kazi ya ualimu katika Shule ya Sekondari ya Southern mkoani Mbeya ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu kishiriki cha elimu Mkwawa (Muce), kilichopo mkoani Iringa.

Mhadhiri huyo ni Dick Aron Mulungu ambaye alisoma na Mulugo katika Shule ya Sekondari ya Songea Wavulana kati ya 1994 na 1996 na alijiunga na shule hiyo baada ya kuhitimu kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Kafule, ambayo iko mkoani Mbeya.
 
Taarifa zinaonyesha kuwa Mulungu alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kupata Shahada ya kwanza katika Elimu (BA Education) 2001 na baadaye alisoma na kupata Shahada ya Uzamili (MA Development studies ) 2007.

Alipotafutwa kupitia simu yake ya mkononi, mahojiano yalikuwa hivi:
Mwandishi: Hallow…(mwandishi akajitambulisha)
Mulungu: Sawa, unasemaje?
Mwanishi: Nazungumza na Dick Mulungu?

Mulungu: Ndiyo mimi.
Mwandishi: Hivi unamfahamu mtu anayeitwa Hamimu Agustino?
Mulungu: Aah… hivi ulisema unaitwa nani?
Mwandishi: Si nimeshajitambulisha jina na ofisi ninayotoka?
Mulungu: Nipigie kesho naona hapa kuna kelele.

Mwandishi: Mbona nakusikia vizuri tu?
Mulungu: Nipigie baada ya nusu saa basi.
Baada ya nusu saa…….
Mwandishi: Haloo… naona nusu saa imekwisha, uko tayari kuzungumza?
Mulungu: Huyo simfahamu.
Mwandishi: Kwani wewe si ulisoma Songea Boys?

Mulungu: Ndiyo
Mwandishi: Kwa hiyo humkumbuki mtu aliyekuwa akitumia jina hilo?
Mulungu: Huyo mtu namkumbuka ndiyo.
Mwandishi: Kwa sasa yuko wapi?
Mulungu: Siwezi kujua, si unajua tumesoma siku nyingi sasa huwezi kujua mtu amekwenda wapi… ni siku nyingi mno.
Mwandishi: Ahsante.

Chuo Kikuu na siasa
Taarifa zinaonyesha kuwa Waziri Mulugo alijiunga na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania 2002 akitumia majina ya Philipo Hamimu Augustino na alisomea Shahada ya Sanaa katika Elimu (BA. Ed). Namba yake ya usajili chuoni hapo ni 08652/T.02.
Alipokuwa akiendelea na kazi ya ualimu Mulugo alianza harakati za kisiasa na ndipo alipoamua kwenda kugombea ubunge katika majimbo ya wilaya ya Chunya.

Kada wa chama cha NCCR Mageuzi wilayani Chunya, Nyawili Kalenda aliyejitambulisha kama mlezi wa siasa wa Waziri huyo alisema walifahamiana naye 2004 wakati Mulugo na rafiki yake walipokwenda kumtaka ushauri wa kugombea ubunge katika jimbo la Songwe.
Katika nakala za wasifu wake zinaonyesha kuwa 2008 alishika nafasi ndani ya CCM ambazo ni pamoja na mjumbe wa baraza la jumuiya ya wazazi wilaya ya Chunya, Katibu wa Elimu, Uchumi, Malezi na mazingira wa jumuiya ya wilaya hiyo na mjumbe wa baraza la wazazi mkoa wa Mbeya.

Kauli yake
Mulugo anasema madai hayo yamekuwa yakitolewa mara kwa mara na amekuwa akiyajibu kwa kuwaonyesha vyeti vyake halali vya shule. “Hayo madai ni ya muda mrefu, wewe sijui utakuwa mtu wa 20 kuuliza swali kama hilo. Mimi vyeti ninavyo na hata ukitaka ushahidi nitakuonyesha,” alisema Waziri Mulugo.

Licha ya kukiri kurudia darasa la saba, Waziri Mulugo alisema jina la Hamimu amekuwa akilitumia katika elimu tangu awali na kwamba hakuvunja sheria kufanya hivyo.

“Jina la Hamim ni la nyumbani Philipo ni jina langu la ubatizo, nadhani haya ni mambo ya kawaida na kweli nilipokuwa shule watu walikuwa wananifahamu kama Hamimu pia Philipo ni jina langu la ubatizo na kumbuka tukifika chuo huwa tunatumia jina la baba.

“Na pia ni kweli nilirudia shule kwa sababu wakati ule wa Mwalimu Nyerere na Mwinyi (Ali Hassan), sheria ilikuwa inaruhusu maana wanafunzi walikuwa wachache mno, fikiria katika darasa letu la saba tulimaliza watu saba tu. Baadaye sheria hiyo ilibadilishwa,” aliongeza.

Kuhusu jina la Dick Mulungu, alikiri kumfahamu mtu huyo na kwamba walisoma wote shule ya Sekondari ya Songea Boys. Hata hivyo, alipinga kutumia vyeti vyake.

“Ni kweli Dick Mulungu tulisoma wote Songea Boys. Lakini hili jina la Mulungu ni jina letu la ukoo. Babu yangu alikuwa akiitwa Filipo Milambo Mulungu, kwa hiyo niliendelea kulitumia hivyo hivyo na hata jina la Mulugo ni letu pia,” alisema.

Endelea: Mwananchi