Pages

Saturday, March 30, 2013

Balaa tena! Watu 40 wahofiwa kufukiwa baada ya jengo la ghorofa 15 kuporomoka Dar

Dar es Salaam. Watu zaidi ya 40 wanahofiwa kufukiwa na kifusi baada ya jengo la ghorofa 16 lililokuwa linajengwa kuporomoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam jana asubuhi.
 
Kuporomoka kwa ghorofa hilo lililokuwa katika Mtaa wa Indira Gandhi, kulizua huzuni, taharuki na simanzi kwa ndugu na jamaa waliofika kwenye eneo la tukio kutaka kufahamu nini kimetokea.
 
Shughuli mbalimbali katikati ya jiji hilo zilisimama kwa siku nzima baada ya jengo hilo kuanguka na kusababisha vifo vya watu watano, 13 kuokolewa huku zaidi ya watu 40 wakisadikiwa kufukiwa na kifusi cha udongo wa jengo hilo.
 
Jengo lililoporomoka
 
Jengo hilo lililokuwa likijengwa mkabala na Msikiti wa Shia Ithnasheri ulioko Barabara ya Indira Gandhi na Kampuni ya ‘Lucky Construction Limited’ lilianguka majira ya saa 2.30 asubuhi wakati ujenzi ukiendelea juu huku chini watoto wakicheza mpira na mama lishe wakiendelea na biashara zao kama kawaida.

Pamoja na vifo na wengine kujeruhiwa, magari takribani manne yalifunikwa na kifusi cha jengo hilo na kupondwa pondwa na kuwa kama chapati.
 
Katibu wa Msikiti wa huo wa Shia Ithnasheri, Mushtaq Damji alisema: “Leo tulikuwa na kitu kama jumuiya kwa jamii ya wahindu, tulipanga kusherehekea lakini yote yakafutika.
 
“Baada ya swala ya alfajiri, watu walikuwa wanazungumza hapa na pale na baada ya kupambazuka, watoto walikuwa wanacheza mpira, walikuwa 9. Sasa, bahati nzuri watoto saba wakakimbia na watoto wawili wakawa wamekwama,” alisema Damji.

Naye Mlinzi wa Msikiti huo, Athuman Nassor alisema: “Mimi nafanya kazi ya ulinzi hapa msikitini, lakini nilikuwa ninashangaa kiasi cha saruji kilichokuwa kikitumika kukorogea zege, kweli walikuwa wanazidisha mchanga.
 
“Niliwahi kuwaambia hata hawa vibarua, kuwa hii inayofanyika mbona siyo…,” alisema mlinzi huyo. Alisema; jana ilikuwa siku ya kumwaga zege ghorofa ya 16 na kulikuwa na vibarua wapatao 50 ambao kila mmoja alikuwa na ndoo yake tayari kuanza kazi kabla ya ghorofa hilo kuporomoka.
Mlinzi huyo alisema kuwa wakati tukio hilo linatokea alikuwa mbali kidogo na eneo la tukio na kusema kuwa bila shaka baadhi ya kinamama lishe ni miongoni mwa waliofukiwa.

Habari zilizopatikana baadaye jana jioni zilidai kuwa mmiliki wa jengo, Ally Raza pamoja na mhandisi wa Kampuni iliyokuwa ikijenga jengo hilo ya Lucky Construction Limited walidakwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere wakijiandaa kutimka.

Viongozi wamiminika
 
Rais Jakaya Kikwete alifika katika eneo la tukio saa 6:45 mchana na alipata maelezo mafupi ya tukio hilo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadik na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
 
Baada ya maelezo hayo, Rais Kikwete aliyetumia dakika tisa, alimwambia Mkuu wa Mkoa na Kamanda Kova: “…mmiliki na mhandisi lazima wakamatwe mara moja.”
Kikwete baadaye alitikisa kichwa kuonyesha masikitiko na kuondoka.
 
Viongozi wengine waliofika ni Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal ambaye hata hivyo hakuzungumza lolote hata baada ya kupata taarifa kutoka kwa mkuu wa mkoa.
 
Naye aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) ambaye sasa ni Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa CCM, Dk Asha-Rose Migiro alisema tukio hilo linaumiza na kusikitisha kwani limepoteza nguvu kazi ya taifa.
 
“Ni vigumu kupata maneno ambayo yatabeba uzito wa tukio hili lakini wajenzi wanatakiwa kuwa makini na ujenzi wao,” alisema Migiro.

Wananchi wajitokeza kuokoa
 
Mapema Wananchi waliojitokeza kwa kushirikiana na askari polisi na mgambo wa Jiji walioanza kuondoa kifusi cha mchanga kwa kutumia mikono kutokana na kutokuwapo kwa vifaa vya kuondolea kifusi hicho.

Endelea: Mwananchi

Thursday, March 28, 2013

Rais Tucta ang’olewa

 
Mambo siyo shwari ndani ya Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) kutokana na kutimuliwa kwa Rais wake, Ayoub Omar.

Omar alilithibitishia gazeti hili jana kuwa aliondolewa wadhifa huo kwenye kikao cha Kamati ya Utendaji cha Tucta kilichofanyika Machi 25, mwaka huu.

Alisema kuwa alivuliwa wadhifa huo baada ya kuundiwa zengwe na viongozi wenzake waliodai asingeweza kuendelea na wadhifa huo kwani hakuwa na sifa.
 
Katiba ya Tucta inaelekeza kuwa kiongozi wake lazima awe mwajiriwa katika sekta ya umma au ile ya binafsi.

Omar alisema kuwa viongozi wenzake walikuja na ajenda kuwa hakuwa na kazi kwani alikuwa amestaafu kwenye Kiwanda cha Mbolea cha Mbeya alikokuwa anafanya kazi.

“Ni kweli nilistaafu pale Kiwanda cha Mbolea lakini nilipata ajira sehemu nyingine baada ya muda mfupi,” alieleza Ayoub, ambaye kwa sasa anafanya kazi kwenye Kampuni ya Nuru Enterprise.

Ayoub alisema alisikitishwa na kitendo kile kwani anaona ni zengwe tu kwani ana sifa za kuongoza kwa kuwa ni mwajiriwa.

“Mimi naheshimu uamuzi wao ila niliwapelekea vielelezo kuwa mimi ni mwajiriwa lakini walikataa,” aliongeza Ayoub, ambaye anaendelea na wadhifa wake kama Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani (Tuico).

Katibu Mkuu wa Tuico, Nicolaus Mgaya alipoulizwa kuhusu suala hilo, alikanusha vikali kuenguliwa kwa mwenyekiti wake.

Gazeti hili, hata hivyo, linafahamu kuwa suala hilo limesababisha mgawanyiko mkubwa ndani ya Tucta.

Source: Mwananchi

Tuesday, March 26, 2013

Cheti alichotumia Mulugo cha Mhadhiri wa Mkwawa

 
Dar es Salaam. Imebainika kuwa mmoja wa watu ambao Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo (pichani)anadaiwa kutumia jina lake kutafuta kazi ya ualimu katika Shule ya Sekondari ya Southern mkoani Mbeya ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu kishiriki cha elimu Mkwawa (Muce), kilichopo mkoani Iringa.

Mhadhiri huyo ni Dick Aron Mulungu ambaye alisoma na Mulugo katika Shule ya Sekondari ya Songea Wavulana kati ya 1994 na 1996 na alijiunga na shule hiyo baada ya kuhitimu kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Kafule, ambayo iko mkoani Mbeya.
 
Taarifa zinaonyesha kuwa Mulungu alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kupata Shahada ya kwanza katika Elimu (BA Education) 2001 na baadaye alisoma na kupata Shahada ya Uzamili (MA Development studies ) 2007.

Alipotafutwa kupitia simu yake ya mkononi, mahojiano yalikuwa hivi:
Mwandishi: Hallow…(mwandishi akajitambulisha)
Mulungu: Sawa, unasemaje?
Mwanishi: Nazungumza na Dick Mulungu?

Mulungu: Ndiyo mimi.
Mwandishi: Hivi unamfahamu mtu anayeitwa Hamimu Agustino?
Mulungu: Aah… hivi ulisema unaitwa nani?
Mwandishi: Si nimeshajitambulisha jina na ofisi ninayotoka?
Mulungu: Nipigie kesho naona hapa kuna kelele.

Mwandishi: Mbona nakusikia vizuri tu?
Mulungu: Nipigie baada ya nusu saa basi.
Baada ya nusu saa…….
Mwandishi: Haloo… naona nusu saa imekwisha, uko tayari kuzungumza?
Mulungu: Huyo simfahamu.
Mwandishi: Kwani wewe si ulisoma Songea Boys?

Mulungu: Ndiyo
Mwandishi: Kwa hiyo humkumbuki mtu aliyekuwa akitumia jina hilo?
Mulungu: Huyo mtu namkumbuka ndiyo.
Mwandishi: Kwa sasa yuko wapi?
Mulungu: Siwezi kujua, si unajua tumesoma siku nyingi sasa huwezi kujua mtu amekwenda wapi… ni siku nyingi mno.
Mwandishi: Ahsante.

Chuo Kikuu na siasa
Taarifa zinaonyesha kuwa Waziri Mulugo alijiunga na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania 2002 akitumia majina ya Philipo Hamimu Augustino na alisomea Shahada ya Sanaa katika Elimu (BA. Ed). Namba yake ya usajili chuoni hapo ni 08652/T.02.
Alipokuwa akiendelea na kazi ya ualimu Mulugo alianza harakati za kisiasa na ndipo alipoamua kwenda kugombea ubunge katika majimbo ya wilaya ya Chunya.

Kada wa chama cha NCCR Mageuzi wilayani Chunya, Nyawili Kalenda aliyejitambulisha kama mlezi wa siasa wa Waziri huyo alisema walifahamiana naye 2004 wakati Mulugo na rafiki yake walipokwenda kumtaka ushauri wa kugombea ubunge katika jimbo la Songwe.
Katika nakala za wasifu wake zinaonyesha kuwa 2008 alishika nafasi ndani ya CCM ambazo ni pamoja na mjumbe wa baraza la jumuiya ya wazazi wilaya ya Chunya, Katibu wa Elimu, Uchumi, Malezi na mazingira wa jumuiya ya wilaya hiyo na mjumbe wa baraza la wazazi mkoa wa Mbeya.

Kauli yake
Mulugo anasema madai hayo yamekuwa yakitolewa mara kwa mara na amekuwa akiyajibu kwa kuwaonyesha vyeti vyake halali vya shule. “Hayo madai ni ya muda mrefu, wewe sijui utakuwa mtu wa 20 kuuliza swali kama hilo. Mimi vyeti ninavyo na hata ukitaka ushahidi nitakuonyesha,” alisema Waziri Mulugo.

Licha ya kukiri kurudia darasa la saba, Waziri Mulugo alisema jina la Hamimu amekuwa akilitumia katika elimu tangu awali na kwamba hakuvunja sheria kufanya hivyo.

“Jina la Hamim ni la nyumbani Philipo ni jina langu la ubatizo, nadhani haya ni mambo ya kawaida na kweli nilipokuwa shule watu walikuwa wananifahamu kama Hamimu pia Philipo ni jina langu la ubatizo na kumbuka tukifika chuo huwa tunatumia jina la baba.

“Na pia ni kweli nilirudia shule kwa sababu wakati ule wa Mwalimu Nyerere na Mwinyi (Ali Hassan), sheria ilikuwa inaruhusu maana wanafunzi walikuwa wachache mno, fikiria katika darasa letu la saba tulimaliza watu saba tu. Baadaye sheria hiyo ilibadilishwa,” aliongeza.

Kuhusu jina la Dick Mulungu, alikiri kumfahamu mtu huyo na kwamba walisoma wote shule ya Sekondari ya Songea Boys. Hata hivyo, alipinga kutumia vyeti vyake.

“Ni kweli Dick Mulungu tulisoma wote Songea Boys. Lakini hili jina la Mulungu ni jina letu la ukoo. Babu yangu alikuwa akiitwa Filipo Milambo Mulungu, kwa hiyo niliendelea kulitumia hivyo hivyo na hata jina la Mulugo ni letu pia,” alisema.

Endelea: Mwananchi

Wednesday, March 20, 2013

Mshichana Pakistan aliyejifanya kuwa mvulana

 
Maria Toorpakai Wazir, mshichana kutoka Waziristan, Pakistan, ambaye kwa miaka kadhaa ilibidi acheze mchezo wa squash akiwa anajidai kuwa mvulana, sasa amekuwa mchezaji shupavu.
Eneo la Waziristan ni eneo ambapo itikadi za Kiisilamu zinafuatwa sana. Kwa hivyo kwa Maria kucheza squash ni jambo la ajabu katika eneo ambalo wasichana hawakubaliwi hata kwenda shule.
 
Lakini Maria anasema, "Mimi ni jasiri. Nilizaliwa jasiri na nitakufa jasiri."
Babake amemuunga kwa dhati Maria kwa kumpa nafasi ingawaje anasema: "Huku kwetu wasichana hawakubaliwi hata kutoka nje wanamoishi."
Kaptula
Squash ni mchezo unaopendwa sana nchini Pakistan. Wanawake pia huucheza, ingawaje siyo eneoni Waziristan au kwenye maeneo mengine yenye itijadi kali.
Toorpakai anasema alipoanza kucheza squash akiwa kavaa kama mtoto wa kiume, si wengi waliogundua kuwa ni msichana. Lakini walipofanya hivyo walianza kumkejeli na kumtukana, lakini hakufa moyo.
Asema babake: "Wakati watu walipomuona Maria na kugundua kwamba alikuwa havai hijab, na kwamba alicheza squash akiwa amevaa kaptula, walishangaa sana na kunilaumu vikali."
Onyo
Barua ilibandikwa kwenye gari lake baba huyo lililomwambia amwachishe mwanae kucheza squash kwa sababu "ilikuwa ni kinyume na itikadi za Kiisilamu na za kabila".
Walimwambia “angeona cha mtema kuni” iwapo asingefanya hivyo.
Lakini alisisitiza kwamba kama watoto wake wa kike walikuwa na shauku la kucheza mchezo wowote ule basi yeye angewaunga mkono.
Baadaye Maria alijitahidi kutafuta mdhamini na akalekea mafunzoni Canada. Kwa sasa ndiye mchezaji wa juu zaidi wa kike nchini Pakistan, na namba 49 duniani.
 
Source: BBC

Wednesday, March 13, 2013

Sakata la kuteswa kibanda...Waziri Membe atajwa

 
JINA la Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimaitafa, Bernard Membe, limeanza kuhusishwa na tukio la kutekwa na kuteswa kikatili na watu wasiojulikana lililomkuta Mhariri Mtendaji Mkuu wa New Habari (2006) Ltd, Absalom Kibanda.

Madai ya kulihusisha jina la Waziri Membe na tukio hilo, yalianza kuzagaa miongoni mwa watu waliofika katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kumjulia hali Kibanda, muda mfupi baada ya kutendewa unyama huo.

Makundi ya watu waliokuwa hospitalini hapo walilioanisha tukio hilo na kauli iliyopata kutolewa na Waziri Membe katika mahojiano ya kipindi cha Dakika 45, kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV, alipoeleza kuwa anao maadui wakubwa 11, wakiwamo waandishi wa habari wawili ambao aliahidi kuwashughulikia.

Ingawa Membe alikutana na shinikizo la watu mbalimbali lililomtaka awataje maadui zake hao 11, wakiwamo waandishi wa habari wawili ambao alikuwa na mpango wa kuwashughulikia, hadi sasa hajapata kufanya hivyo, jambo ambalo linadaiwa na wadadisi wa mambo kuwa ni uamuzi wake wa kuchukua mkondo wa kutekeleza kile alichokisema kwa vitendo.

Tamko lake hilo katika kipindi hicho kilichorushwa hewani Julai 16, 2012, ambalo limeibua hali ya sintofahamu, sasa linaonekana kuchukuliwa kwa uzito zaidi na wanahabari na wamiliki wa vyombo vya habari, baada ya kuwa moja ya mambo mazito yaliyozungumzwa jana katika mkutano wa wamiliki wa vyombo vya habari.

Kwa takribani siku mbili, Membe amekuwa akitafutwa na gazeti hili kwa ajili ya kuzungumzia madai hayo, lakini hata hivyo jitihada za kuzungumza naye hazikufanikiwa, baada ya simu yake kuita wakati wote bila majibu.

Hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maneno kupitia simu yake ya kiganjani, hakujibu, licha ya kuonyesha umefika.

Jana katika mkutano huo wa wamiliki wa vyombo vya habari ulioketi Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, kujadili kuzorota kwa mazingira ya usalama ya waandishi na wanaharakati wengine, suala hilo la Membe pia lilijadiliwa.

Wakijibu maswali ya waandishi waliotaka kujua namna viongozi wa serikali na watendaji wa vyombo vya ulinzi na usalama wanavyohusishwa na matukio ya aina hii, wamiliki hao walieleza kuwa wapo baadhi ya watendaji waandamizi wa serikali waliokwishalitangazia taifa kuwa wanao maadui 11 hapa nchini, wawili kati ya hao ni waandishi wa habari walioahidi kuwashughulikia.

Akizungumza kwa niaba ya wamiliki wenzake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Hussein Bashe, alisema ni jambo la kushangaza kuona kauli kama hiyo iliyotolewa na kiongozi mwandamizi wa serikali haijafanyiwa kazi na vyombo vya ulinzi na usalama.

“Mfano, mwaka jana, alinukuliwa mwanasiasa na kiongozi wa Serikali kupitia kipindi cha Dakika 45, akisema kuwa ana maadui 11 ambao kati yao, wawili ni waandishi wa habari, hivi kauli hii ambayo ilikuwa ikiruka katika kituo cha luninga haikusikika au adui mwenyewe kati ya waliotajwa ndiyo Kibanda?

“Kama ni hivyo, mbona haitwi ili ahojiwe kuhusu hali hii na vyombo hivi vya ulinzi na usalama vya nchi yetu, tunahitaji kuona kuwa Serikali yetu inafanya kazi na hata kulinda maisha ya watu wake,” alidai Bashe.

Sehemu ya kauli ya Waziri Membe katika kipindi hicho kilichokuwa kikiongozwa na mtangazaji Selemani Semunyu, ambayo sasa inaonekana kuwa hatari kwake, alisema: “Lazima watu hao wajue kwamba ukikaa juu ya nyoka, ipo siku atakugonga tu. Hili nawaachia Watanzania waamue, lakini kuna watu 11, wakiwamo waandishi wawili wa habari, nitawatwanga kweupe.”

Kutokana na hali ya kuzorota huko kwa usalama, hususan wa wanahabari, wamiliki hao waliazimia kuundwa kwa kamati ya watu 16 ambayo itakutana na vyombo vya usalama nchini kuzungumzia kwa undani wa tukio hilo na usalama wa makundi yanayolengwa na vitendo vya kushambuliwa, kuumizwa na hata kuuawa kwa waandishi.

Maazimio mengine yaliyofikiwa katika mkutano huo ni kuitaka serikali kuunda tume huru ya wapelelezi kuchunguza undani wa sakata hilo, kwa sababu kasi ya upelelezi wa vyombo vya usalama vya hapa nchini hairidhishi na kwamba baadhi ya watendaji ndani ya vyombo hivyo wanahusishwa na matukio haya ya utesaji na utekaji.

Aidha, katika kikao hicho, wanachama wa MOAT ambao walisoma tamko lao kwa waandishi wa habari baada ya kumaliza kikao chao, walisema pamoja na kuwepo kwa vitendo vya kuwatesa na kuwaua waandishi, bado ukweli utasimama katika jamii.

Wamiliki hao, ambao waliachiana zamu kusoma tamko lao, walisema vyombo vya usalama kudaiwa kuhusika na vitendo vichafu dhidi ya rais ni udhaifu.

Mmoja wa wajumbe hao, Reginald Mengi, akisoma moja ya maazimio ya mkutano huo, alisema kumekuwa na tishio dhidi ya wanahabari, huku akimtaka Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kutaja maofisa wa vyombo vya ulinzi waliokwenda nyumbani kwa mwandishi wa habari, Eric Kabendera na kuwatisha wazazi wake.

“Tunajua wazi jambo hili lilipangwa na watu ambao wamekuwa wakitumia fedha hata za ufisadi ili kutishia uhai wa waandishi wa habari, kutokana na matukio haya yaliyojitokeza namuomba Waziri Nchimbi awataje maofisa hao, kama asipofanya hivyo tutawataja kwa majina mchana kweupe.

“Pamoja na hila na vitimbi vinavyofanywa na watumishi hao wa idara za ulinzi na usalama dhidi ya wanahabari, ni vema Serikali ichukue hatua za haraka ili kuondoa hali hii. Hivi sasa Watanzania wamekuwa wakiishi kwa woga na katu huwezi kusema nchi ina amani huku watu wake wakitishwa.

“Ninapenda kusema kuwa kwa matukio haya ya kupigwa na kuteswa kwa Kibanda na hili tukio la wazazi wa Kabendera kuhojiwa kule Bukoba, ni wazi hata wakituua watakaobaki watasema ukweli wa nini kilichopo sasa,” alisema Mengi.

Mengi ambaye ni Mwenyekiti wa MOAT, pia alitumia fursa hiyo kutangaza majina ya kamati itakayokutana na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama, kuwa ni pamoja na yeyé mwenyewe ambaye ni mwenyekiti wa kamati hiyo, wajumbe ni Hussein Bashe, Tido Mhando, Aga Mbuguni, Abdallah Mrisho, Ansbert Ngurumo, Mikidadi Mahamud, Pili Mtambalike, Godfrida Jola, Tumaini Mwilenge na Deodatus Balile.

Wengine ni Katibu Mkuu wa Jukwaa la Wahariri nchini, Neville Meena, Samson Kamalamo, Henry Muhanika, Japhet Sanga na Jesse Kwayu.

Alisema wadau hao, mbali na kukutana na Waziri Nchimbi, pia watakutana na Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi, Saidi Mwema, Mkuu wa Usalama wa Taifa, Othuman Rashid na Naibu wake, Jack Zoka pamoja na Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Dk. Edward Hosea.
 
Source: Mtanzania

Sunday, March 10, 2013

Kibanda afanyiwa upasuaji


Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (Tef), Absalom Kibanda ambaye amelazwa Hospitali ya Millpark, Johannesburg nchini Afrika Kusini kutokana na kupata majeraha makubwa baada ya kushambuliwa na watu wasiojulikana, ameng’olewa jicho.
 
Taarifa iliyotolewa na Katibu wa Tef, Neville Meena inaeleza jana aliingizwa kwenye chumba cha upasuaji katika hospitali hiyo, kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji na kurekebishwa sura.

“Nachukua fursa hii kuwapa maendeleo ya tiba ya Mwenyekiti wa Tef Absalom Kibanda, ambaye amelazwa Hospitali ya Millpark, Johannesburg nchini Afrika Kusini, leo ameingizwa theater (chumba cha upasuaji) ili kuanza kufanyiwa upasuaji na kurekebishwa sura, baada ya kupungua kwa uvimbe katika majeraha aliyokuwa nayo sehemu mbalimbali za mwili wake, hususan kichwani na usoni,” alisema Meena katika taarifa yake hiyo.

Meena alifafanua kuwa upasuaji huo unazingatia matokeo ya uchunguzi uliofanywa kwa zaidi ya saa 48 na jopo la madaktari, ambao walibaini kwamba mbali na madhara ya awali, Kibanda pia aliumizwa taya lake la kushoto.

“Kuhusu jicho lake la kushoto ambalo pia lilijeruhiwa, madaktari walisema wangetoa uamuzi kuhusu aina ya upasuaji ambao wangeufanya baada ya kubaini hali halisi, wakati watakapokuwa wakirekebisha sura yake ambayo iliharibiwa kwa majeraha,” alisema.

Alisema Kibanda ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd ambao ni wachapishaji wa magazeti ya Rai,
Mtanzania, Dimba na Bingwa, bado ana maumivu makali kutokana na majeraha aliyopata, kwani hata wakati akipelekwa kwenye upasuaji huo uliotarajiwa kuchukua saa zaidi ya nne, alikuwa akilalamika kwa maumivu zaidi kwenye kidonda kilichopo kwenye mguu wake wa kushoto.

“Tutaendelea kufahamishana kila hatua ya tiba ya mwenyekiti wetu, na tunaomba tuendelee kumwombea ili apone haraka,” alisema Meena.

Juzi jopo la madaktari wanaomtibu katika hospitali hiyo walibaini madhara zaidi aliyoyapata Kibanda, kutokana na unyama aliofanyiwa na watu wasiojulikana usiku wa kuamkia Jumatano wiki hii.
Madhara hayo ni pamoja na kukatika kwa mshipa unaounganisha pua na mdomo, kulegea kwa meno sita, awali ilibainika kuwa ametobolewa jicho lake la kushoto, kung’olewa meno mawili, kunyofolewa kucha, kukatwa mara tatu kwenye kichwa chake.

Katika hatua nyingine, Rais Jakaya Kikwete jana alimtembelea Kibanda hospitalini alikolazwa akiongozana na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.

Meena alisema Rais Kikwete amesema Serikali itajitahidi kuwasaka waliohusika na tukio la utesaji wa Kibanda, ili wafikishwe mahakamani kwa mujibu wa sheria.

Rais Kikwete na Kinana wapo Afrika Kusini kwa ziara ya kikazi, ambapo waliamua kutumia fursa hiyo kwenda kumtembelea mhariri huyo.

Hadi Kibanda anasafirishwa kwenda Afrika Kusini Alhamisi wiki hii kwa matibabu zaidi, viongozi wa Serikali waliofika kumjulia hali ni pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hussein Mwinyi pamoja na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, wahariri na waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari nchini.

Source: Mwananchi